` VICTOR MKWIZU AREJESHA FOMU YA UDIWANI KATA YA NGOKOLO

VICTOR MKWIZU AREJESHA FOMU YA UDIWANI KATA YA NGOKOLO



Na Mapuli Kitina Misalaba

Aliyekuwa Diwani wa Kata ya Ngokolo, Victor Mkwizu, amerejesha rasmi fomu yake ya kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuwania tena nafasi ya udiwani wa kata hiyo katika uchaguzi mkuu ujao.

Mkwizu ambaye amehitimisha kipindi chake cha uongozi wa miaka mitano, amesema ameamua kurejea tena kwa nia ya kuendeleza misingi ya maendeleo aliyoweka pamoja na wananchi wa Ngokolo katika kipindi kilichopita.

“Nimerudi kwa sababu bado nina ndoto ya kuiona Ngokolo ikisonga mbele zaidi. Tumefanikisha mambo mengi, lakini bado kuna mengi ya kufanya. Naamini kwa ushirikiano na wananchi, tunaweza,” amesema Mkwizu mara baada ya kurejesha fomu.

Ameongeza kuwa anayo dhamira ya dhati ya kuendelea kutumikia wananchi kwa moyo wa uzalendo, huku akiahidi kuzingatia maadili ya uongozi, ushirikiano na uwazi katika utekelezaji wa majukumu. 
Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464