Header Ads Widget

OPERESHENI YA POLISI YANASA PIKIPIKI 825 ZA WIZI WATUHUMIWA 354 KANDA YA ZIWA


Na Damian Masyenene - Shinyanga Press Club blog
Jeshi la Polisi nchini kupitia kitengo maalum cha operesheni cha jeshi hilo limetangaza matokeo ya operesheni maalum ya kudhibiti vitendo vya kiuhalifu ikiwemo wizi wa Pikipiki kwa mikoa Nane ya Kanda ya Ziwa, ambapo jumla ya mali/pikipiki 825 zidhaniwazo kuwa za wizi zilikamatwa na kesi 354 kufunguliwa dhidi ya watuhumiwa waliokamatwa.


Matokeo ya opreresheni hiyo ya takribani mwezi mmoja iliyoanza Mei 4 hadi 29, mwaka huu  ikihusisha mikoa nane ya Mwanza, Geita, Shinyanga, Simiyu, Tabora, Tarime/Rorya, Mara na Kagera, imetangazwa leo Mei 30, 2020 jijini Mwanza katika taarifa kwa vyombo vya habari na Mkuu wa Operesheni maalum za jeshi la polisi, SACP Mihayo Msikhela.

SACP Msikhela amesema kuwa hali ya usalama katika mikoa hiyo imeendelea kuwa shwari kutokana na juhudi kubwa inayofanywa na Jeshi hilo kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama pamoja na raia wema.
Taarifa hiyo pia imefafanua namna mashauri ya operesheni yalivyoshughulikiwa kwa kila mkoa, ambapo Tabora (43), Mwanza (19), Simiyu (36), Shinyanga (19), Tarime/Rorya 38), Mara (09), Geita (97) na Kagera (92) na kufanya jumla ya kesi zilizofunguliwa kufikia 353, kesi zilizopelekwa mahakamani (60), kesi zilizopata mafanikio (12), kesi zilizofungwa polisi (16), kesi zilizo chini ya upelelezi (287), pikipiki zilizotozwa faini (241), huku magari sita yakikamatwa.

“Mwanza walikamatwa watuhumiwa 12 na injini za boti 106 katika visiwa vya Juma, Gembale na Zilagula wilayani Sengerema, Tabora wamekamatwa watatu wa mauaji, Geita wamekamatwa watuhumiwa wawili wa wizi wa matairi manne ya Gari aina ya Toyota Surf  T 477 ACY. Katika kufanikisha tukio hilo watuhumiwa walitumia bajaji namba MC 688 BXA TVS KING kwenye ubebaji wa tairi hizo nayo pia imekamatwa na inashikiliwa ili taratibu za kisheria ziweze kufuatwa,” amesema Kamanda Msikhela.

Vile vile, amebainisha baadhi ya mambo kadhaa yaliyobainika katika operesheni hiyo kuwa ni wamiliki wengi wa vyombo vya moto hususani pikipiki hawana uelewa wakutosha kuhusu umiliki, utunzaji, kuazima na hata kukodisha kwa mfano mmiliki anamkabidhi mtu pikipiki bila mikataba au kumjua kiundani anayemkodisha au abiria wake.

“Watu wanachonga namba za pikipiki ilhali hawana vibali au leseni za kufanya kazi hizo, mfano kwa mkoa wa Mara wamekamatwa watuhumiwa watatu wanaohusika na kuchonga namba za pikipiki.

Jeshi la Polisi linatoa rai kwa wananchi wote kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu mapema kabla madhara hayajatokea kwani wahalifu wapo kwenye jamii zetu, hivyo jamii inapaswa kuuchukia uhalifu ili nchi yetu iwe na amani,” amesema.