` TBN YATOA SALAAM ZA MIAKA 64 YA UHURU: YASISITIZA AMANI, UMOJA NA UJENZI WA TAIFA

TBN YATOA SALAAM ZA MIAKA 64 YA UHURU: YASISITIZA AMANI, UMOJA NA UJENZI WA TAIFA


 Tanzania Bloggers Network(TBN) imetoa salamu maalum kwa Watanzania katika kuadhimisha miaka 64 ya Uhuru wa Tanzania Bara, ikisisitiza umuhimu wa amani, utulivu na mshikamano kama nguzo kuu za maendeleo ya Taifa.

Katika salamu hizo zilizotolewa na Mwenyekiti wa TBN Beda Msimbe, ameeleza maadhimisho ya Uhuru si tu siku ya mapumziko, bali ni fursa ya kutafakari safari ya Taifa tangu kupatikana kwa Uhuru mwaka 1961 na kuelewa wajibu wa kizazi cha sasa katika kuendeleza misingi iliyoachwa na waasisi wa nchi.

TBN imemrejea Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyewahi kusisitiza kuwa:

“Uhuru hauwezi kukamilika pasipo kujitegemea. Hatuwezi kuitwa huru kama tunategemea wengine kutupatia mahitaji yetu ya kimsingi.”

Mtandao huo umesema kauli hiyo bado ina uzito mkubwa kwa kizazi cha leo, hasa katika zama za uchumi wa kidijitali, ambapo ubunifu, bidii na ushirikiano vina nafasi kubwa katika kuleta maendeleo.

Jukumu la Watanzania: Kulinda Amani na Kuepuka Uchochezi

Katika ujumbe huo, TBN imesisitiza kuwa mafanikio yaliyofikiwa na Taifa ni matokeo ya utulivu na umoja uliodumu kwa miongo kadhaa. Mtandao huo umeonya kuwa vurugu, chuki na uchochezi vinaweza kuyumbisha juhudi za miaka mingi za kupambana na adui ujinga, umaskini na maradhi.

Rais mstaafu Benjamin William Mkapa aliwahi kusema:“Amani si kitu cha asili, tunahitaji kuilinda na kuitunza kila siku. Bila amani, hakuna maendeleo ya kweli.”

TBN imetumia kauli hiyo kuwakumbusha Watanzania kuwa mustakabali wa Taifa uko mikononi mwa wao wenyewe.

 Kuheshimu Zama na Mwelekeo wa Uongozi

Mtandao huo pia umeangazia umuhimu wa kuheshimu mchango wa kila awamu ya uongozi nchini, ukimnukuu Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi aliyesema:

“Kila utawala na zama zake. Kila kiongozi na mchango wake katika ujenzi wa Taifa hili.”

TBN imesisitiza kuunga mkono falsafa ya 4R inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan — Reconciliation, Resilience, Reforms, and Rebuilding — inayolenga kuimarisha umoja wa Taifa, mageuzi na ustawi wa wananchi.

Wito kwa Vijana na Watanzania Wote

TBN imewataka Watanzania kutumia uhuru wa kutoa maoni kwa busara na siyo kama silaha ya kubomoa Taifa. Mtandao huo umesisitiza kuwa,Uhuru ni wajibu,Amani ni nguzo ya maendeleo na Kujituma  kufanya kazi kwa bidii ndilo deni kwa waasisi wa nchi.

TBN inawatakia Watanzania wote maadhimisho mema ya miaka 64 ya Uhuru,

“Tanzania Kwanza. Kazi na Utu, Tusonge Mbele.”

 

  

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464