` CHEREHANI USHETU IMEBADILIKA NICHAGUENI TENA NISIMAMIE MIRADI NA KUTATUA CHANGAMOTO ZOTE.

CHEREHANI USHETU IMEBADILIKA NICHAGUENI TENA NISIMAMIE MIRADI NA KUTATUA CHANGAMOTO ZOTE.

Na Kareny  Masasy, Ushetu

MGOMBEA Ubunge kupitia chama cha Mapinduzi (CCM) jimbo la Ushetu  Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga Emanuel Cherehani   amesema wananchi  waendelee kumuamini na kumchagua ili aweze kukamilisha miradi  iliyotengewa fedha na serikali  ambayo inaendelea kutekelezwa na kuendelea  kutatua changamoto zingine   ikiwemo  suala la kilimo.

Pia  amesema   Serikali imetoa shilingi  Bilioni 156 kwa jimbo hilo   kwaajili ya shughuli za Maendeleo ikiwemo ujenzi wa vyumba vya madarasa, miundombinu ya barabara na kuweka nishati ya Umeme ambavyo vyote amevipigania  na fedha kupatikana.

Cherehani amesema  hayo tarehe 13.Septemba,2025 kwenye uzinduzi wa Kampeni wa jimbo hilo uliofanyika  kijiji cha  Iramba kata ya Igwamanoni ambapo alieleza  jimbo hilo lina kata 20,vijiji 122 na vitongoji 550  ikiwa aliingia madarakani mwaka 2021 mwezi Oktoba baada ya  mbunge aliyekuwepo kufariki alikuta vijiji 70 tu ndiyo vina nishati ya Umeme.

Cherehani amesema  serikali  ilileta shilingi Bilioni 156 kwa nyakati tofauti kwaajili ya kutatua kero za wananchi  kwani kuna mradi wa  sola unaogharimu shilingi Bilioni 11.7 unaoendelea kujengwa kijiji cha  Kayenze na wakandarasi bado wanaendelea na kazi na tayari kuna sola zaidi ya 200 zipo tayari.

"Mpaka sasa vijiji vyote 112 vina nishati ya umeme  na baadhi  ya vitongoji hivyo tupeni kura chama cha Mapinduzi wagombea wote wa Udiwani, Ubunge na Rais  tutekeleze yale  ambayo tumeanza nayo na kuyakamilisha na  lengo  la kuwa na mradi mkubwa wa Sola  tunataka kila kitongoji kuwe na umeme kuongeza nguvu ya umeme uwe wa uhakika  maeneo yote."amesema Cherehani.

Cherehani amesema  zaidi ya  shilingi Bilioni 9.2 zimeletwa na serikali jimboni hapo na kujenga vyumba vya madarasa 230  na shilingi  Milion 540 zimejenga shule ya sekondari Mweri ya wasichana na hakuna mwananchi aliyechangishwa fedha zake na watoto wanasoma vizuri.

Cherehani amesema  bado kuna changamoto ya miundombinu ya barabara kuwa mibovu ambapo jimbo hilo walipata shilingi Milioni 600 kwaajili  kuweka Molamu baadhi ya barabara na endapo wananchi wakimpatia ridhaa ya kuongoza tena atahakikisha  barabara za kuunganisha kutoka kijiji kimoja kwenda kingine zinaboreshwa zaidi na kupitika kirahisi.

Mgombea diwani wa kata ya Igwamanoni Gagi Lala amesema  vijiji vyote saba  vina  nishati ya umeme,kuna zahanati mbili na kituo cha afya kimoja, lakini zahanati zingine zinajengwa mbili nakufikisha hospitali  tano ndani ya kata moja , maji ya kisima kirefu ndiyo wanatumia  ni kazi ya  Chama Cha Mapinduzi ambayo imetekeleza ilani yake na itaendelea kutekeleza wakiichagua.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa amesema  ilani ya chama imeeleza vizuri kila changamoto inakwenda kutekelezwa hivyo wachague chama hicho na wagombea wake kwani ilani itatekelezwa kwa kuwachagua wote wanaotokana na chama hicho na mambo makubwa yamefanyika yanaonekana ndani ya mkoa huu ikiwemo Ruzuku ya mbolea kwa wakulima.



Mkazi wa kata ya Nyamilangano Sawaka  Sagenge  amesema  wanachotaka viongozi watakao chaguliwa mwaka huu wahakikishe changamoto zinaenda kutatuliwa  kwani  wanahitaji  barabara  yenye urefu wa kilomita 54 iwe ya lami inayotoka kwenye kata hiyo hadi mjini Kahama kwani ina kiwango cha changarawe ambayo ndiyo kiungo kikuu kwenye jimbo hili.

Mkazi wa Kitongoji cha kipangu kata Igwamanoni  Gaudensia  Mahushi amesema  viongozi watakao wachagua wanaomba nishati ya umeme kwenye kitongoji hicho  kwani umeme umeishia kwenye kijiji pekee  na miundombinu ya barabara mibovu wakitaka kwenda kijiji jirani wanazunguka hakuna barabara kabisa hata wakiwa wanakwenda kwenye Zahanati ni changamoto.




 

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464