` FADHILI NAFUTARI ATANGAZA NIA YA KUGOMBEA UBUNGE JIMBO LA ITWANGI,AAHIDI KUINUA KILIMO, MADINI NA UCHUMI WA WANANCHI

FADHILI NAFUTARI ATANGAZA NIA YA KUGOMBEA UBUNGE JIMBO LA ITWANGI,AAHIDI KUINUA KILIMO, MADINI NA UCHUMI WA WANANCHI


Mtia nia ya kugombea Ubunge Jimbo la Itwangi Fadhili Nafutari 

Na Mwandishi wa Shinyanga Press Club Blog

 Fadhili Salmon Nafutari, Mtanzania mzalendo na kijana mwenye maono ya kweli ya maendeleo, ametangaza rasmi nia yake ya kugombea nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Itwangi, Wilaya ya Shinyanga akiwa na msukumo wa kulijenga jimbo hilo kupitia rasilimali zake za asili na nguvu kazi ya wananchi wake.

  Fadhili anakuja na dira mpya ya maendeleo yenye kugusa maisha ya kila mwananchi,ambapo katika  hotuba yake ya kutangaza nia amesema Itwangi ni miongoni mwa maeneo ya Shinyanga yenye utajiri mkubwa wa rasilimali, hasa madini na ardhi yenye rutuba, lakini bado fursa hizo hazijawanufaisha kikamilifu.

 “Itwangi ina madini wananchi wake wanahitaji kupimiwa maeneo yao rasmi ili waweze kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za uchimbaji, kuanzisha vikundi vya uchimbaji wa pamoja, na kupewa elimu juu ya thamani ya madini wanayoyapata kwa kufanya hivi, tutaondoa unyonyaji na kuwawezesha wananchi wetu kupata kipato halali na cha kudumu,” amesema Fadhili.

 Mbali na Sekta ya madini, Fadhili amesema suluhisho la kudumu kwa changamoto ya kilimo ni kuchimba na kuendeleza marambo ya maji kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji,kutokana na kuwa na maeneo mengi yanayofaa kwa uchimbaji wa mabwawa ya maji (marambo) ambayo yakitumika vyema yatawezesha wakulima kulima kwa msimu wote na kujiongezea kipato.

 “Tutachimba marambo ya maji kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji hili litasaidia wakulima kuondokana na utegemezi wa mvua na kuongeza uzalishaji hata kipindi cha kiangazi na itaimarisha usalama wa chakula na kuinua pato la familia nyingi za wakulima,” ameongeza.

 Ajenda Kuu za Fadhili Nafutari kwa Jimbo la Itwangi moja ni kuendeleza Sekta ya Madini kwa kupima maeneo ya madini, kuwawezesha wachimbaji wadogo, kuanzisha saccos na vikundi vya vijana na wanawake kwenye sekta hiyo.

  Jambo la pili ni kuhakikisha wananchi wanalima kilimo cha Umwagiliaji kupitia marambo ya maji yatakayochimbwa na ujenzi wa miundombinu rafiki ya kilimo cha kisasa ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi,na tatu ni  kuwezesha Vijana na Wanawake Kiuchumi  elimu ya  ujasiriamali, mikopo ya vikundi na kuunganisha na taasisi za fedha kwa maendeleo endelevu.

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464