Header Ads Widget

RC TELACK AONGOZA SHEREHE ZA 'MEI MOSI' SHINYANGA, AWASIHI WAFANYAKAZI KUMPA NAFASI RAIS SAMIA....WAFANYAKAZI BORA WATUNUKIWA

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack (wa pili kushoto) akikabidhi zawadi na vyeti kwa baadhi ya wafanyakazi bora mkoani humo, ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha sikukuuya wafanyakazi. Hafla hiyo imefanyika leo katika Ukumbi wa CCM mkoa wa Shinyanga

Na Shinyanga Press Club Blog
SHIRIKISHO la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Shinyanga limeeleza kuridhika na ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan kupandisha watumishi madaraja na mishahara mwakani.

TUCTA Shinyanga wameeleza hayo leo Mei 4, 2021 katika kongamano la muendelezo wa siku ya wafanyakazi duniani lililoambatana na kutunuku vyeti na zawadi kwa wafanyakazi bora mwaka 2020/2021, ambapo baadhi ya wafanyakazi wameonyesha kuwa na imani na Rais Samia Suluhu Hasan kwa ahadi yake aliyoitoa katika sherehe za Mei Mosi kitaifa jijini Mwanza.

Akitoa kauli hiyo, Mwenyekiti wa TUCTA mkoa wa Shinyanga, John Balele ametoa wito kwa mabaraza ya kazi yaliyofikia ukomo kuhuishwana na mengine mapya kufunguliwa, huku akiwahimiza waajiri wawe waaminifu na waadilifu.

Balele ameongeza kwa kueleza kuwa ameridhishwa na utoaji wa zawadi kwa wafanyakazi bora ambazo zinawapa motisha wafanyakazi na kuwataka waajiri kutenga zawadi zaidi kwa wafanyakazi bora ili kuongeza hamasa na ufanisi katika maeneo ya kazi.

Akiwasilisha salamu za wafanyakazi kwa Rais Samia Suluhu Hassan kupitia mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Sekta ya Afya (TUGHE) mkoa wa Shinyanga, Allan Isaya amesisitiza umoja baina ya sekta binafsi na umma kwa kutenga fedha za kutoa zawadi kwa wafanyakazi bora.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack amewataka wafanyakazi kumpa nafasi Rais Samia Suluhu Hassan kufanyia kazi ahadi alizotoa ikiwemo kupandisha mishahara na madaraja huku akiwataka maofisa utumishi kuandaa mapema orodha ya wafanyakazi wanaostahili kupanda madaraja.

RC Telack ametumia nafasi hiyo kukemea tabia ya baadhi ya waajiri wenye tabia ya kutoa zawadi hewa kwa wafanyakazi wao katika sherehe za Mei Mosi.

"Maofisa utumishi mnapaswa kuhakikisha mnatoa kwa wakati stahiki za wafanyakazi, muandae mapema orodha ya watumishi wanaostahili kupanda madaraja na kazi hiyo ifanywe kwa weledi na uaminifu mkubwa.

"Tutaendelea kushirikiana kwa pamoja na watumishi wa sekta zote na serikali inawategemea kwa kiasi kikubwa ili kuusaidia mkoa wetu kupiga hatua. Wafanyakazi mmpe nafasi Rais Samia Suluhu Hassan na kusubiri ahadi yake na pia mfanye kazi kwa bidi bila kinyongo," amesisitiza.

TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack akizungumza na wafanyakazi na kuwasisitiza kufanya kazi kwa bidii bila kinyongo ili kumpa nafasi Rais Samia Suluhu Hassan kutimiza ahadi yake kwao
Mwenyekiti wa TUCTA mkoa wa Shinyanga, John Balele akieleza namna tuzo na vyeti kwa wafanyakazi hao vitakavyoleta motisha na ufanisi kazi
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Sekta ya Afya (TUGHE) mkoa wa Shinyanga, Allan Isaya akitoa salamu za wafanyakazi hao kwa Rais Samia mbele ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack (hayupo pichani)
Mmoja wa wafanyakazi, Julius Shagama akieleza namna ambavyo wana imani na ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kutimiza ahadi yake kwa wafanyakazi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba (kulia) pamoja na wadau wengine wakishuhudia sherehe hizo
Wafanyakazi wa kada mbalimbali wakiwa kwenye sherehe hizo
Wafanyakazi wakishuhudia matukio mbalimbali katika hafla hiyo
Wafanyakazi wa kada ya ualimu wakiwa ni sehemu ya sherehe hizo
Wafanyakazi wakiendelea kufurahia katika sherehe hizo
Sherehe zikiendelea
Wafanyakazi wakifurahia matukio mbalimbali katika sherehe hiyo
Zawadi Mbalimbali zikikabidhiwa kwa baadhi ya wafanyakazi bora




Post a Comment

0 Comments