Header Ads Widget

'MAZINGIRA MAZURI YACHANGIA KUKUA KWA MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI'


Katibu Mkuu Dkt. John Jingu akizungumza wakati wa kufungua mafunzo ya Wasajili wasaidizi wa NGOs ngazi za Mikoa na Halmashauri kutoka mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Tanga yanayofanyika Jijini Dar es salaam kwa siku mbili tarehe 3 na 4 Septemba, 2020.

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
Kutokana na Serikali kuboresha mazingira ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali (NGOs) kufanya kazi, mashirika hayo yameendelea kukua siku hadi siku kwa kusaidiana na Serikali katika sekta mbalimbali.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya - Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Dkt. John Jingu wakati akifungua mafunzo kwa Wasajili wasaidizi wa NGOs ngazi za Mikoa na Halmashauri kutoka Mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Tanga yanayoendelea Jijini Dar es salaam.

Dkt. Jingu amesema Serikali imekuwa ikiandaa mazingira wezeshi kwa NGOs kufanya kazi kwa tija ili ziweze kutoa mchango kwa maendeleo ya nchi. 

"Mazingira haya mazuri ndiyo yanaiwezesha sekta ya NGOs kukua na kustawi siku hadi siku na kutoa mchango katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo sekta ya ajira" amesema Jingu.

Amesema katika kuboresha mazingira hayo, zimeundwa sheria, sera na kanuni mbalimbali ili kuendana na mazingira yaliyopo ikiwemo kuwezesha mashirika hayo kusimama kama Taasisi zinazojisimamia.

Dkt. Jingu amewasisitiza Wasajili wasaidizi kuhimiza uwazi na uwajibikaji kwa lengo la kuifanya sekta hii kuaminika kwa wananchi na mchango wake uwe na thamani kwa jamii.

"Uwazi na uwajibikaji ni Msingi imara ya utawala bora na nchi yetu imejikita katika kujenga misingi ya utawala bora kwenye nyanja zote ikiwemo Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Lengo tujue mchango wa mashirika haya nchini" aliongeza Dkt. Jingu.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi Dkt. Laurean Ndumbaro amewataka washiriki kusimamia Sheria, Taratibu, Kanuni na miongozo ya uendeshaji wa NGOs katika maeneo yao sambàmba miongozo na maadili ya utumishi wa Umma.

"NGOs zisaidie kujenga uzalendo zaidi kwa Watanzania wanaoheshimu mila na tamaduni zao "Muangalie shughuli wanazozifanya ziendane na malengo ya nchi yetu" amesisitza Dkt. Ndumbaro.

Aidha, Dkt. Ndumbaro amewataka wasajili wakumbuke sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa Umma katika majukumu yao ya Usajili wa NGOs.

"Kuwateua kuwa wasajili wasaidizi ni kuzingatia matakwa ya kanuni za utumishi wa Umma, hivyo mambo mengi yanawaongoza katika usajili wenu hasa sheria, sera ya NGO, kanuni zinazoongoza utendaji wa NGOs pamoja na miongozo inayotolewa na Wizara ya Afya chini ya Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii" amesisitiza Dkt. Ndumbaro.

Awali, Msajili wa NGOs, Vickness Mayao amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao Wasajili wasaidizi walioteuliwa ili kuhakikisha jamii iliyokusudiwa inapata maendeleo.

Amesema Serikali katika kusimamia uratibu wa mashirika hayo imefanya maboresho mbalimbali katika sheria, kanuni na kuandaa muongozo wa uratibu wa mashirika yasiyo ya Kiserikali, mabadiliko hayo yameenda sambamba na uteuzi wa wasajili wasaidizi katika ngazi za Mikoa na Halmashauri.

Mwenyekiti wa Bodi ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Dkt. Richard Sambaiga akitoa neno la shukrani, amesema wasajili wanawajibika kufahamu taasisi yoyote inayoingia kwenye maeneo yao.

"Sisi ni kama mabalozi, isije taasisi kwenye Idara yoyote bila sisi kuwa na taarifa"
 Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi Dkt. Laurean Ndumbaro akizungumza na Wasajili wasaidizi wa NGOs wakati wa mafunzo kwa Wasajili hao ngazi za Mikoa na Halmashauri kutoka Mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Tanga yaliyofanyika Jijini Dar es salaam.
  Mwanasheria kutoka Ofisi ya Msajili wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali Faki Shaweji akitoa mada kuhusu dhana, sheria na kanuni za mashirika yasiyo ya Kiserikali kwa Wasajili wasaidizi wa ngazi za Mikoa na Halmashauri wa Mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Tanga waliopata mafunzo yanayofanyika jijini Dar es salaam
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Wasajili wasaidizi wa NGOs ngazi za Mikoa na Halmashauri wa Mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Tanga wakifuatilia mada katika mafunzo hayo jijini Dar es salaam.
Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali Vickness Mayao akifafanua jambo kwa washiriki wa mafunzo ya Wasajili Wasaidizi wa NGOs wa Mikoa na Halmashauri za Dar es salaam, Morogoro na Tanga yaliyofanyika jijini Dar es salaam.

Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini (WAMJW)