Header Ads Widget

16 WAFIKISHWA MAHAKAMANI SONGWE TUHUMA ZA MAUAJI YA KADA WA CCM

 
 Watu 16 wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Songwe juzi, wakikabiliwa na shtaka la mauaji ya anayedaiwa kuwa ni kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Briton Mollel.

Mauaji hayo yalitokea baada ya kuzuka vurugu kati ya watu wanaodaiwa kuwa wafuasi wa CCM na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kusababisha watu wengine wawili kujeruhiwa.

Waliofikishwa mahakamani ni Peter Charahani, Ijumeleghe Mwanjila, Elia Sichone, Charles Simkonda, Daudi Mwajunga, Wiliam Simkoko, Oscar Philip, Yohana Mkumbwa, Feston Kitta, Tonny Siwale na Ayubu Mwakasege.

Wengine ni James Simkoko, Julius Wilson, Emmanuel Msinjili, Hidaya Mwangoka na Jenifer Mwasenga.

Wakili wa Serikali, Renatus Mkude, alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Kassim Mkwawa, kuwa watuhumiwa walitenda kosa hilo Agosti 25, mwaka huu katika eneo la kata ya Mwakakati Mji wa Tunduma wilayani Momba, mkoani Songwe.

Akiwasomea shtaka hilo katika kesi hiyo ya jinai , Wakili Mkude alidai kuwa washtakiwa kwa pamoja walitenda kosa hilo la kuua kinyume cha kanuni ya adhabu Sura ya 16 ya Sheria za Tanzania.

Hakumu Mkwawa aliiahirisha kesi hiyo hadi Septemba 14, mwaka huu, ambapo watuhumiwa walirudishwa mahabusu kwa sababu kesi hiyo haina dhamana.