Header Ads Widget

RAIS MAGUFULI AWAAPISHA VIONGOZI WAPYA, AWASISITIZA KURIDHIKA NA VYEO VYAO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli

Na Damian Masyenene – Shinyanga Press Club Blog
LEO Julai 16, 2020 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli amewaapisha viongozi wapya wakiwemo wakuu wa mikoa, wilaya, wakurugenzi na makatibu tawala aliowateua jana (Jumatano), ambapo amewasisitiza kuridhika na vyeo vyao, kuwa wavumilivu na kwenda kutatua kero za wananchi katika maeneo yao ya kazi.

Hafla hiyo ya kuwaapisha viongozi hao imefanyika Ikulu ya Chamwino, jijini Dodoma ikihudhuriwa pia na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri wa Tamisemi, Selemani Jafo na wakuu mbalimbali wa mikoa na vyombo vya usalama.

Moja ya nukuu alizozitoa leo Rais Magufuli ni ‘Katika kazi hizi kuridhika ni kitu muhimu sana’, ambapo aliwatolea mfano viongozi mbalimbali wapya aliowaapisha leo ambao wamekuwa wavumilivu na wariridhika na nyadhifa zao, akiwemo Mkuu mpya wa Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, Dkt. Seleman Serera ambaye ana Shahada udhamivu (PhD) na alikuwa anapokea mshahara wa Sh 500,000 akaridhika na sasa amepanda cheo.

“Najaribu kutoa mifano hii ili wanaotusikiliza watuelewe, nendeni mkafanye kazi katika maeneo yenu mkavumilie. Huko mnakokwenda mnakwenda kutekeleza ilani ya CCM kwahiyo kila mmoja katika eneo lake akafanye kila anachoona kinafaa kwa manufaa ya nchi na kuwaletea maendeleo wananchi wa eneo husika.
.
“Tukazingatie maadili, tukachape kazi, msiende kuchukua muda mrefu wa kujifunza ama kuzoea kazi….mkurugenzi wa TIC kahakikishe tunapata wawekezaji wengi, tusiwazungushe wawekezaji, tunahitaji wawekezaji, kwahiyo nikuombe Dokta kahakikishie mwenyekezaji anayekuja leo anapata fursa,” amesema.

Pia Rais Magufuli amewapongeza wale wote waliojitokeza kuwania nafasi mbalimbali ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo amewaomba kukazingatia nidhamu na maadili ya chama hicho.

“Niwathibitishie tu kwamba hakuna mtu yeyote aliyetumwa na mimi, waziri mkuu, makamu wa rais, kama kuna watu wanazungumza kwamba mimi nimewatuma ni uongo.

“Sababu naskia wanasema eti wametumwa na Rais, sasa kama nimekutuma kwanini nihangaike kukutuma, si ningesubiri tu kwenye uteuzi wa viti 10 nikakuteua,” amesema.