Header Ads Widget

RC TELACK AZITEMBELEA SHULE ZA KIDATO CHA SITA KISHAPU, AAGIZA WANAFUNZI WASIBANANISHWE MABWENINI


       Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack (wa pili kulia) akizungumza na wanafunzi wa kidato cha sita katika shule ya sekondari Kishapu alipofanya ziara kujionea utayari wa shule hiyo kupokea wanafunzi waliorejea kuanza masomo. 

Na Catherine Ngowi - Kishapu

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack amewataka viongozi wa shule za sekondari hususan zilizopokea wanafunzi wa kidato cha sita walioanza masomo Juni mosi, mwaka huu, kuendelea kuchukua tahadhari kwa kuweka mazingira mazuri ambayo yatawafanya wasibanane mabwenini kwani ugonjwa wa COVID-19 bado upo.

Mkuu huyo wa mkoa amesisitiza pia wanafunzi kuendelea kufundishwa njia bora za kujikinga dhidi ya ugonjwa huo ikiwemo kunawa mikono kwa usahihi na kuweka miundombinu yote inayohitajika kwa ajili ya kuchukua tahadhari, huku maofisa elimu nao wakitakiwa kushirikiana na walimu katika kipindi hiki.

RC Telack ametoa maagizo hayo leo Juni 2, 2020 wilayani Kishapu mkoani hapa baada ya kuzitembelea na kuzikagua shule za sekondari Shinyanga na Kishapu zenye wanafunzi wa kidato cha tano na sita alipokuwa akikagua hali ya maandalizi kwa shule hizo dhidi ya ugonjwa wa COVID-19 unaoambukizwa na virusi vya Corona.

“Nia yetu ni kuhakikisha kuwa mnakuwa salama, wanafunzi wakipata maambukizi na nyie walimu mtapata, jikingeni kwa sababu Corona ipo. Pia katika mabweni yao ya kulala hakikisheni wanapata nafasi za kutosha wasibanane. Nanyi Maafisa elimu shirikianeni na walimu katika kipindi hiki cha Corona kutatua changamoto katika shule hizi,” amesema RC Telack.

Aidha Mkuu wa Mkoa amewataka wanafunzi kusoma kwa bidii kwa kushirikiana pamoja ili kujiandaa vyema na mitihani ijayo, huku akiagiza uongozi wa shule hizo kuhakikisha wanafunzi wanakula chakula bora na kwa wakati ili kufanya vyema katika masomo yao.

“Someni kwa pamoja kwa sababu tunataka wote mtoke mkiwa mmefaulu hivyo mshirikiane na msaidiane kwenye masomo angalau kila mtu aweze kufaulu kwenda chuo kikuu. Sasa hivi acheni kulala, tumieni huu muda uliobaki vizuri kwa sababu hatutaki daraja la tatu wala sifuri, nataka kuona kila mtu akipata daraja la kwanza,” amesisitiza Mkuu wa Mkoa.

Kulingana na ratiba iliyotolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia chini ya Waziri mwenye dhamana Profesa  Joyce Ndalichako,  wanafunzi wa kidato cha sita wanatarajia kuanza mtihami wa taifa Juni 29, 2020.



Post a Comment

0 Comments