Header Ads Widget

AGAPE YAWAKUMBUKA WALEMAVU YATOA KIFAA CHA KISASA CHA KUNAWIA MIKONO

ma



Shirika la Agape (ACP) linalotetea haki za wanawake na watoto mkoani Shinyanga, limewataka wananchi mkoani humo kuwakinga watu wenye ulemavu na maambukizi ya virusi vya Corona hasa wasioona, pale wanapokuwa wakihitaji msaada wa kuwashika mkono na kuwavusha kwenye vivuko vya barabara.
Hayo yamebainishwa leo Juni 3,2020, na mkurugenzi wa Shirika hilo John Myola, wakati akikabidhi kifaa cha kunawa mikono kwa sabuni na majitiririka kwenye ofisi ya chama cha watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata), pamoja na kuwapatia elimu ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.

Myola amesema watu wenye ulemavu hasa wasioona wapo katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya virusi vya Corona, sababu mara nyingi hua wanahitaji msaada wa watu kuwavusha barabara na nilazima washikwe mikono, hivyo endapo mtu huyo hakunawa mikono ama kujipata Sanitize atakuwa katika hatari ya kumuambukiza.

“Natoa wito kwa wananchi mkoani Shinyanga na maeneo mengine hapa nchini, tuwalinde watu hawa wenye ulemavu hasa wasiiona, pale tunapokuwa tukiwapatia msaada mbalimbali ikiwamo kuwavusha barabarani, tuzingatie unawaji mikono ama kujipaka Sanitize, ili kuwahakikishia usalama wao wasipate maambukizi ya virusi vya Corona,”amesema Myola.

“Sisi kama Agape tumeguswa na kundi hili maalum, na ndio maana tumeamua kuwapatia kifaa hiki cha kunawa mikono kwa sabuni na majitiririka kwenye ofisi yao, pamoja na kuwapatia elimu ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona ili waendelee kubaki salama,” ameongeza.

Kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata) Richard Mpongo, amepongeza Shirika hilo kwa kuwajali na kuwapatia kifaa hicho pamoja na elimu ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona, jambo ambalo limewafanya kufarijika na wataendelea kujilinda.

Aidha amewataka wananchi mkoani humo kutowanyanyapaa watu hao wenye ulemavu hasa katika kipindi hiki cha Janga la maambukizi ya virusi vya Corona, bali pale wanapokuwa wakihitaji msaada wao wahakikishe wananawa mikono au kujipaka vitakasa mikono (Sanitize) ndipo wawashike mikono ili wote wabaki kuwa salama.


TAZAMA PICHA HAPA CHINI


Mkurugenzi wa Shirika la Agape mkoani Shinyanga , akitoa elimu ya kujikinga na Maambukizi ya virusi vya Corona kwa watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata).

Mkurugenzi wa Shirika la Agape mkoani Shinyanga John Myola akitoa elimu wa watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata) namna ya uvaaji wa barakoa na kuzivua ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.

Afisa mradi wa utu wa msichana kutoka Shirika la Agape Sophia Rwazo akitoa elimu ya kujikinga na virusi vya Corona kwa watu wenye ulemavu.

Mkurugenzi wa Shirika la Agape mkoani Shinyanga John Myola, akitoa elimu namna ya kunawa mikono kwa sabuni na majitiririka ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.

Zoezi la unawaji mikono likiendelea kwa sabuni na majitiririka.

Zoezi la unawaji mikono likiendelea kwa sabuni na majitiririka.

Mwenyekiti wa chama cha watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata) Richad Mpongo, kushoto, akinawa mikono kwa sabuni na majitiririka mara baada ya kupewa mafunzo na kifaa hicho ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.

Katibu wa chama cha watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata) Uel Nyange, akinawa mikono kwa sabuni na majitirika mara baada ya kupewa mafunzo na kifaa hicho ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.

Mwenyekiti wa chama cha watu wenye Ualbino mkoani Shinyanga Unisi Zabron Manumbu, akinawa mikono kwa sabuni na majitiririka.

Mwenyekiti wa chama cha watu wenye ulemavu mkoani Shinyanga (Shivyawata) Richard Mpongo akishukuru utolewaji wa elimu kwao namna ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona , pamoja na kifaa cha kujikinga na Maambukizi ya virusi hivyo.

Na Marco Maduhu- Shinyanga.