Header Ads Widget

WATANZANIA 192 WALIOKUWA WAMEKWAMA NCHINI INDIA WAREJEA NCHINI


Serikali yarejesha kwa awamu ya pili Watanzania 192 waliokuwa wamekwama nchini India kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19.

Ubalozi wa Tanzania nchini India kwa kushirikiana na Shirika la Ndege la Tanzania [ATCL] pamoja na Diaspora wa Tanzania nchini India kwa mara nyingine wamefanikisha safari ya pili ya kuwarejesha nchini Watanzania 192 waliokuwa wamekwama katika miji mbalimbali nchini India. 

Watanzania hao walikwama kutokana na zuio la kuingia na kutoka kwa ndege za Kimataifa lililowekwa na Serikali ya India kama hatua mojawapo ya kudhibiti kuenea kwa maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19.

Ndege maalum ya aina ya Boeng 787-8 ya Dreamliner ya Shirika la Ndege la Tanzania ilitumwa tena na Serikali Jijini Mumbai kuja kuwachukua Watanzania hao waliokwama nchini India tangu tarehe 22 Machi 2020 lilipowekwa zuio hilo na Serikali ya India. 

Ndege hiyo iliondoka tarehe 30 Mei 2020 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Chhatrapati Shivaji,  Mumbai ikiwa imebeba jumla ya raia wa Tanzania 192, miongoni mwao ni waliokuwa wamekwenda India kwa ajili ya matibabu; wahitimu kutoka vyuo mbali mbali na wanafunzi ambao wanalazimika kurudi nyumbani kwa kuwa vyuo vimefungwa hadi mwezi Agosti/Septemba 2020.

Tofauti na awamu ya kwanza, safari hii pia ilihusisha kuwarejesha nchini India raia wa nchi hiyo wapatao 202 ambao walikuwa wamekwama nchini Tanzania. Hatua hii ya Serikali ya Tanzania itasaidia sana katika kuimarisha mahusiano mazuri yaliyopo kati ya India na Tanzania.

Mpaka sasa jumla ya Watanzania 438 wamerejeshwa Tanzania kutoka India kwa utaratibu huu maalum.