` WANANCHI SHINYANGA WAHIMIZA SUBIRA NA AMANI WAKATI TUME YA RAIS IKIENDELEA NA UCHUNGUZI

WANDAMAN HOTEL

WANANCHI SHINYANGA WAHIMIZA SUBIRA NA AMANI WAKATI TUME YA RAIS IKIENDELEA NA UCHUNGUZI

Wakazi wa Manispaa ya Shinyanga wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kuzingatia utulivu na mshikamano wa kitaifa wakati Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2025, ikiendelea na kazi yake ya kukusanya maoni na ushahidi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mahojiano, wananchi hao wameeleza kuwa mchakato huo ni hatua muhimu ya kujenga maridhiano ya kweli na kurejesha imani miongoni mwa jamii, wakisisitiza kuwa mafanikio ya tume yanategemea ushirikiano wa wananchi wote.

Chibura Makorongo mkazi wa Manispaa hiyo, amesema kuundwa kwa tume hiyo kunaashiria nia ya dhati ya viongozi wa nchi kusikiliza kilio cha wananchi na kushughulikia changamoto zilizojitokeza kwa uwazi na haki.

Kwa mujibu wa Makorongo, historia ya Tanzania kama taifa lenye amani inapaswa kulindwa kwa vitendo, akieleza kuwa juhudi za kusikiliza pande zote kupitia tume ni njia mojawapo ya kudumisha heshima hiyo ndani na nje ya nchi.

Naye mkazi mwingine Peter Omari amesema  mazungumzo ya wazi ndiyo msingi wa suluhu ya kudumu, akibainisha kuwa kila mwananchi anapaswa kutumia fursa hiyo kueleza yaliyompata ili kusaidia kupatikana kwa ukweli.

Akichangia hoja hiyo, Joramu Mihayo wa eneo la Kambarage amesema kuwa mshikamano wa kitaifa unahitaji moyo wa kuvumiliana na kusameheana badala ya kutumia nguvu.

Kwa upande wake Pendo Herman mkazi wa  Mtaa wa Ngokolo amesema hatua ya serikali kuunda tume hiyo imeleta matumaini mapya kwa wananchi, hususan wale walioguswa na matukio hayo ambapo amesema kila Mtanzania anapaswa kutambua kuwa amani ni nguzo kuu ya maendeleo, hivyo inapaswa kulindwa kwa vitendo kupitia ushiriki katika mchakato wa maridhiano.

 

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464