` AMANI NI UHAI WA TAIFA: DEREVA BODA BODA SHINYANGA ATOA WITO WA KUDUMISHA UTULIVU

WANDAMAN HOTEL

AMANI NI UHAI WA TAIFA: DEREVA BODA BODA SHINYANGA ATOA WITO WA KUDUMISHA UTULIVU

Afisa usafirishaji wa bodaboda, Shabani Adam, mkazi wa Manispaa ya Shinyanga, ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kulinda na kuthamini amani iliyopo nchini, akieleza kuwa hatamani kuona hali ya utulivu ikitoweka kwa namna yoyote ile.

Akizungumza kwa hisia, Shabani amesema kuwa amani ni nguzo muhimu ya maisha ya kila siku, akisisitiza kuwa hakuna furaha ya kweli kwa mtu au jamii endapo hakuna utulivu wa ndani ya moyo na katika taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa Watanzania wanapaswa kumshukuru Mungu kwa kuijalia nchi yao hali ya umoja, mshikamano na amani, ambayo imewawezesha kuishi na kufanya shughuli zao za kiuchumi bila hofu wala bughudha.

Kwa mujibu wa Shabani, mchango wa vyombo vya ulinzi na usalama ni mkubwa katika kuhakikisha wananchi wanaendelea kuishi kwa amani, Amesema majeshi hayo yamekuwa mstari wa mbele kulinda usalama wa raia na mali zao, jambo linalowafanya wananchi kujivunia nchi yao.

Aidha, ameiomba serikali kuendelea kuviimarisha vyombo hivyo ili viweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, akibainisha kuwa uwekezaji katika usalama wa taifa ni uwekezaji katika ustawi wa wananchi wake.

Shabani pia amesisitiza kuwa hatamani kuona vurugu za aina yoyote zinatokea, iwe ni kati ya wananchi wenyewe, kati ya wananchi na serikali, au hata baina ya mataifa, akieleza kuwa migogoro huathiri kwa kiasi kikubwa maendeleo na ustawi wa jamii.

Amehitimisha kwa kusema kuwa uhuru uliopo watanzania wa kufanya kazi mchana na usiku bila hofu ni jambo la kujivunia, hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha amani hiyo inadumu milele kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

  

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464