` KITUMBO ATOA WITO WA KUILINDA AMANI KWA MAENDELEO YA TAIFA

WANDAMAN HOTEL

KITUMBO ATOA WITO WA KUILINDA AMANI KWA MAENDELEO YA TAIFA

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Salum Kitumbo   

Na Stella Herman, Shinyanga

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Salum Kitumbo amewahimiza Watanzania kuendelea kuthamini na kuilinda amani iliyopo nchini kwa kutumia vyema muungano wa Tanganyika na Zanzibar kama msingi wa mshikamano wa kitaifa.

 Amesema kuwa umoja huo ni nguzo muhimu inayochangia utulivu wa nchi na kuleta mshikamano ambao umewezesha taifa kuwa na utulivu mkubwa ambao unatakiwa kuendelea kulindwa.

Akizungumza wakati wa mahojiano maalum,Kitumbo amesisitiza kuwa bila kuwepo kwa amani, hakuna shughuli yoyote ya maendeleo inayoweza kufanyika kwa ufanisi. Ameeleza kuwa mazingira ya utulivu ndiyo yanayowezesha watu kufanya kazi, kuendesha biashara na kujiletea maendeleo yao binafsi na ya taifa kwa ujumla.

Aidha, amewataka wananchi kutambua kuwa amani waliyonayo si jambo la bahati mbaya, bali ni matokeo ya juhudi na misingi imara iliyowekwa na waasisi wa taifa huku akiwakumbusha kuwa ni jukumu la kila Mtanzania kuilinda na kuidumisha kwa vitendo, ili vizazi vijavyo viweze kuendelea kufurahia utulivu huo.

Kitumbo amewataja viongozi waasisi kama Julius Kambarage Nyerere na Abeid Amani Karume kuwa walitoa mchango mkubwa katika kuijenga Tanzania yenye umoja, mshikamano na amani kwa  kuweka msingi wa taifa linalojali utu, haki na usawa.

Pia alisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kujituma katika kazi na shughuli za uzalishaji, kwani kufanya kazi kwa bidii ndiyo msingi wa maendeleo ya kweli, kwani taifa lenye amani lakini lisilo na juhudi za kiuchumi haliwezi kufikia malengo yake ya maendeleo.

Meya Kitumbo ametoa wito kwa Watanzania wote kuendelea kushikamana, kuheshimiana na kulinda tunu ya amani, akisisitiza kuwa amani ni msingi wa kila jambo jema na bila hivyo hakuna maendeleo yatakayoweza kupatikana. 
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Salum Kitumbo


Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464