` AMANI NA UFAHAMU WA HAKI ZA MIKOPO: NGUZO YA USTAWI WA TAIFA

WANDAMAN HOTEL

AMANI NA UFAHAMU WA HAKI ZA MIKOPO: NGUZO YA USTAWI WA TAIFA

Imeelezwa kuwa ustawi wa taifa unahitaji utulivu na amani ili kuwawezesha wananchi kufanya shughuli za maendeleo kwa ufanisi na kuchochea ukuaji wa uchumi,ikiwa ni pamoja na kumaliza migogoro ambayo inaweza kujitokeza kwenye Jamii ambayo ni chanzo kikubwa cha kuzorotesha maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Akizungumza katika mahojiano maalum kuhusu haki na wajibu wa mkopeshaji na mkopaji Naibu Katibu Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania(LRCT) Zainab Chanzi, amesisitiza umuhimu wa wananchi kuelewa misingi ya sheria katika masuala ya mikopo ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima na kuwawezesha kuwa na utulivu.

Amesema kuwa migogoro mingi inayojitokeza katika jamii inatokana na ukosefu wa uelewa wa haki na wajibu kati ya mkopeshaji na mkopaji, Hivyo, ni muhimu kwa kila upande kujitambua na kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa makubaliano na sheria zilizopo ili kudumisha uhusiano mzuri na kuimarisha amani.

Chanzi ameongeza kuwa uelewa huo ni muhimu hasa katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya taifa ya dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambayo inalenga kuwa na taifa lenye amani, mshikamano na ustawi wa kiuchumi huku akibainisha kuwa  bila kuwepo kwa msingi imara wa haki na uaminifu katika mikopo, ni vigumu kufikia maendeleo endelevu.

Amesema migogoro inababisha kuchelewa kwa ukuaji wa uchumi na kudhoofisha jitihada za wananchi katika kujikwamua kiuchumi,hali hiyo inahitaji elimu endelevu kwa jamii ili kuwajengea uwezo wa kufanya maamuzi sahihi wanapoingia katika mikataba ya kifedha hatua ambayo italeta maridhiano mazuri.

Amesema wajibu wa mkopaji ni  kuhakikisha anazingatia masharti ya mkopo, huku mkopeshaji naye akifuata misingi ya haki, uwazi na uadilifu katika utoaji wa huduma hiyo ili kuleta utulivu na kuendelea kujenga upendo na amani.

 Ametoa wito kwa wananchi kuzingatia elimu ya kifedha na kisheria ili kupunguza migogoro inayotokana na mikopo hasa kwa taaisisi za fedha zilizopewa dhamana hiyo, kwa kufanya hivyo, taifa litaweza kujenga mazingira bora ya amani, utulivu na maendeleo endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464