
Imeelezwa kuwa ustawi wa taifa unahitaji utulivu na amani ili kuwawezesha wananchi kufanya shughuli za maendeleo kwa ufanisi na kuchochea ukuaji wa uchumi,ikiwa ni pamoja na kumaliza migogoro ambayo inaweza kujitokeza kwenye Jamii ambayo ni chanzo kikubwa cha kuzorotesha maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Akizungumza katika mahojiano maalum kuhusu
haki na wajibu wa mkopeshaji na mkopaji Naibu Katibu Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania(LRCT) Zainab Chanzi, amesisitiza umuhimu wa wananchi
kuelewa misingi ya sheria katika masuala ya mikopo ili kuepusha migogoro isiyo
ya lazima na kuwawezesha kuwa na utulivu.
Amesema kuwa migogoro mingi inayojitokeza
katika jamii inatokana na ukosefu wa uelewa wa haki na wajibu kati ya
mkopeshaji na mkopaji, Hivyo, ni muhimu kwa kila upande kujitambua na
kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa makubaliano na sheria zilizopo ili
kudumisha uhusiano mzuri na kuimarisha amani.
Chanzi ameongeza kuwa uelewa huo ni muhimu
hasa katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya taifa ya dira ya Taifa ya mwaka
2050 ambayo inalenga kuwa na taifa lenye amani, mshikamano na ustawi wa
kiuchumi huku akibainisha kuwa bila
kuwepo kwa msingi imara wa haki na uaminifu katika mikopo, ni vigumu kufikia
maendeleo endelevu.
Amesema migogoro inababisha kuchelewa kwa
ukuaji wa uchumi na kudhoofisha jitihada za wananchi katika kujikwamua
kiuchumi,hali hiyo inahitaji elimu endelevu kwa jamii ili kuwajengea uwezo wa
kufanya maamuzi sahihi wanapoingia katika mikataba ya kifedha hatua ambayo
italeta maridhiano mazuri.
Amesema wajibu wa mkopaji ni kuhakikisha anazingatia masharti ya mkopo,
huku mkopeshaji naye akifuata misingi ya haki, uwazi na uadilifu katika utoaji
wa huduma hiyo ili kuleta utulivu na kuendelea kujenga upendo na amani.
Ametoa
wito kwa wananchi kuzingatia elimu ya kifedha na kisheria ili kupunguza
migogoro inayotokana na mikopo hasa kwa taaisisi za fedha zilizopewa dhamana
hiyo, kwa kufanya hivyo, taifa litaweza kujenga mazingira bora ya amani,
utulivu na maendeleo endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.