Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga, Patrobas Katambi, amewashukuru wananchi wa Jimbo la Shinyanga pamoja na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali kwa usimamizi mzuri wa uchaguzi uliowezesha kupatikana kwa madiwani, wabunge na Rais.
Katambi ameyasema hayo leo Februari 22,2026 wakati akizungumza na viongozi wa CCM kutoka kata zote za Wilaya ya Shinyanga katika mkutano maalum wa kuwashukuru wananchi kwa ushiriki wao mkubwa katika uchaguzi, ambapo amesema wananchi na viongozi wa CCM walifanya kazi kubwa ya kupiga kura na kuleta ushindi wa kishindo.“Lengo la kuwaita leo ni kuwashukuru
kwa kazi kubwa mliyoifanya, Niwaahidi tutasimamia miradi yote ya maendeleo na
haki za wananchi wote bila kumuonea mtu yeyote, kwani tunasimamia misingi ya
kikatiba,” amesema Katambi.
Ameeleza kuwa yeye pamoja na
madiwani na wabunge wana jukumu la kuwaletea wananchi maendeleo na kuhakikisha
miradi yote inatekelezwa kwa ufanisi. Amesisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya
Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan
imetoa fedha nyingi za maendeleo, hivyo amewataka wakandarasi kufanya kazi kwa
wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.
“Sitakubaliana na mkandarasi yeyote
atakayochelewesha kazi bila sababu maalum. Fedha zipo, kazi ifanyike,”
amesisitiza.
Katambi pia ameeleza kuwa hatakubali
siasa za mipasuko, chuki za kisiasa au kidini, akisisitiza kuwa amani ni msingi
wa maendeleo na lazima ilindwe kwa maslahi ya wananchi wote.
“Tunataka haki na amani kwa kila
mmoja. Changamoto zozote za kisiasa au kidini tutazishughulikia kwa mujibu wa
sheria,” ameongeza.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM
Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa,
amewataka wananchi na viongozi wa CCM kumuombea Waziri Katambi, akieleza kuwa
anatekeleza jukumu kubwa la kitaifa linalohitaji maombi na mshikamano.
Amesema ushindi mkubwa uliopatikana
Shinyanga Mjini umeleta matunda makubwa kwa Mkoa wa Shinyanga, na amewataka
wananchi kuendelea kumpa ushirikiano ili aweze kutekeleza majukumu yake
ipasavyo.
“Tuache ushabiki wa majungu,Uchaguzi
umeisha, sasa ni wakati wa kuwa wapambe wa maendeleo CCM ni moja, na lazima tuendelee kulinda amani
ya nchi yetu,” amesema Mlolwa.
Aidha, amewataka madiwani wote wa Mkoa wa Shinyanga kwenda kwa wananchi kuwashukuru kwa kuwaamini na kuwachagua kwa kura nyingi, akisisitiza kuwa ni wajibu wa viongozi kurejesha shukrani kwa wananchi waliowapa dhamana.






































