` GRUMETI FUND YAJIVUNIA KUWA CHACHU YA MABADILIKO CHANYA KWA VIJANA ZAIDI YA ELFU 18 MKOANI MARA

GRUMETI FUND YAJIVUNIA KUWA CHACHU YA MABADILIKO CHANYA KWA VIJANA ZAIDI YA ELFU 18 MKOANI MARA

 

SHIRIKA la Grumeti Fund kupitia Idara ya Maendeleo ya jamii limejivunia mafanikio yake katika kubadili fikra za vijana zaidi ya elfu 18 ndani ya Mkoa wa Mara kupitia elimu ya kijinsia inayotolewa na Shirika hilo katika Wilaya za Serengeti na Bunda Mkoani Mara kwani elimu hiyo imeonesha kuwa na tija miongoni mwa jamii hizo.

Taarifa iliyotolewa na shirika  hilo imeeleza kuwa elimu ya kijinsia imekuwa na  tija kubwa miongoni mwa jamii za Wilaya za Serengeti na Bunda, hasa kwa kuwapa vijana uelewa mpana kuhusu masuala ya jinsia, kujitambua na usawa kwani matunda ya elimu hiyo yameonekana husasni katika jamii ambazo mwanzo ziliaminika kutompa kipaumbele mtoto wa kike katika masuala ya elimu.

Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii kutoka Grumeti Fund Bi. Frida Mollel akizungumza katika hafla ya kuwakaribisha wageni kutoka nchi mbalimbali waliotembelea Shirika la Grumeti Fund kama hatua ya kushuhudia,kuunga mkono na kusherekea jitihada za Shirika hilo katika kuwapa mabinti elimu ya kujitambua maarufu kama (SERENGETI GIRLS RUN) amesema wageni hao wamekuja kuunga mkono jitihada za Grumeti Fund ili kupata nguvu zaidi na kutanua wigo katika kumkomboa mtoto wa kike katika maeneo mbalimbali hususani katika kupata haki ya elimu na mahitaji muhimu wakati wa hedhi.

Bi. Frida amesisitiza kuwa programu hii imekuwa na lengo la kujenga kizazi cha vijana wenye uelewa kuhusu umuhimu wa usawa wa kijinsia, kuheshimu utu, na kufanya maamuzi sahihi kuhusu afya ya uzazi na kusema kuwa mafanikio haya yanaonesha jinsi uwekezaji katika elimu ya kijinsia unavyoweza kuwa na athari chanya na ya kudumu katika kuboresha maendeleo ya jamii.

Aidha Bi. Frida ameongeza kuwa Grumeti Fund inajivunia miaka nane ya makongamano mbalimbali ambayo yamekuwa yakiendeshwa na Shirika hilo kwani yameonesha mabadiliko makubwa katika jamii sambamba na kuwapa nguvu watoto wa kike na wa kiume katika kupambania ndoto zao na kubadili mitazamo hasi katika jamii na kutoa wito kwa jamii kuzingatia usawa baina ya mtoto wa kike na wa kiume ili kujenga jamii endelevu na yenye usawa.

"Kwa miaka takribani nane Grumeti Fund imekuwa ikiongea na kutoa fursa kwa  vijana kushiriki kutoa mawazo yao ni kwa jinsi gani wanaweza kuzishinda changamoto zinazowakabili. Tumekuwa  tukiwashauri na kuonesha umuhimu wao katika jamii ili waje kuwa kizazi bora kwani tunaamini kwamba jamii yenye usawa ndani yake ni jamii yenye maendeleo, leo mabinti wameonesha jinsi ambavyo wamenufaika na semina zetu, hii kwetu sisi kama Grumeti Fund haya ni mafanikio makubwa sana ukilinganisha na tulipo toka, kupitia program zetu hivi sasa watoto wa kike na kiume wanapata fursa sawa za Elimu na Afya kwani halikuwa jambo rahisi katika jamii zetu" alisema Bi. Frida 

Kwa upande wa wanafunzi wa kike walioshiriki hafla hiyo wameeleza mafanikio makubwa waliyopata kupitia semina mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa na Grumeti Fund na kueleza namna ambavyo zimebadisha fikra zao na kuamsha ari na ujasiri katika kupambania ndoto zao na kuhamasisha usawa katika jamii.

Kwa takribani Miaka  nane Shirika la Grumeti Fund limekuwa likitoa elimu ya kijinsia kwa wanafunzi wa kike na kiume katika shule za sekondari mbalimbali Wilayani Serengeti na Bunda ambapo tangu mwaka 2017 hadi kufikia Mwaka huu 2025 limefanikiwa kutoa elimu ya kijinsia kwa wasichana (18, 513 ) na kutoa taulo (18,536) kwa kila binti anayeshiriki mafunzo hayo, huku ikifanikiwa kutoa mafunzo kwa wavulana zaidi ya (8791) tangu mwaka 2017 hadi mwaka huu 2025 na kutoa zawadi za jezi na mipira  kwa kila shule iliyoshiriki kwenye kongamano.  




















Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464