Header Ads Widget

MADIWANI WAMKATAA MENEJA WA TANESCO SHINYANGA


Madiwani wa halmashauri ya Shinyanga wakiwa kwenye kikao cha baraza.


Mkurugenzi ha halmashauri ya Shinyanga Nice Municy akijibu hoja za madiwani kwenye kikao cha baraza la madiwani.

Diwani wa kata ya Itwangi Sonya Jilala akizungumza kwenye kikao cha baraza la madiwani.
Mhandisi mkuu wa Tanesco Kulwa Mangara akijibu hoja za madiwani jana kwenye kikao cha baraza.

Na Suzy Luhende, SHINYANGA

Madiwani wa halmashauri ya Shinyanga mkoani hapa, wamesema hawamtaki Meneja wa Tanesco mkoa Grace Ntungi kwa sababu hawatendei haki katika kuwaunganishia umeme katika maeneo yao, ikiwa ni pamoja na kutofatilia pindi wanapotoa taarifa za kuibiwa fedha wananchi wakati wanapolipia malipo ya umeme, hivyo wamesema aondolewe.

 

Hayo wameyasema jana wakati wakitoa hoja mbalimbali kwenye kikao cha baraza la madiwani lililofanyika katika halmashauri hiyo, ambapo walisema meneja huyo amekuwa akiwachonganisha madiwani na wananchi kwa kuwapelekea nguzo za umeme kisha kuzihamisha kuzipeleka vijiji vingine.

Diwani wa kata ya Itwangi Sonya Jilala amesema, hivi karibuni walipokea nguzo katika kijiji cha Butini na Kidanda na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema alifika kijiji hicho na kuwapongeza kuwa wananchi watapata umeme hivi karibuni kwa sababu tayari nguzo zimeshapelekwa, lakini baada ya siku chache nguzo hizo zikaondolewa na kupelekwa sehemu nyingine.


"Baada ya kuondolewa wananchi wakabaki wakitulalamikia kuwa ina maana zililetwa nguzo hizo aje kuziona mkuu wa mkoa halafu waziondoe,pia kwa nini walimsababisha mkuu wa mkoa aongee uongo kwa wananchi, maana aliwapongeza Tanesco na kuwataka wananchi wakae mkao wa kufanya maendeleo kwa sababu umeme umeshawafikia, hatufai kabisa huyu mama pamoja na timu yake aondolewe"amesema Jilala.


"Pia nilitoa taarifa za kuibiwa fadha watu wangu watatu walioibiwa laki tisa tisa kila mmoja kwa ajili ya kuunganishiwa nguzo za umeme, lakini sijaona meneja akilifuatilia jambo hili ni kimya tu, hivyo hatuoni msaada wake na hatuioni kazi anayoifanya maana kila diwani mwenye kata yake hapa anamlalamikia hakuna anachokifanya hafai kabisa"amesema Sonya.
 

Diwani wa kata ya Ilola Amos Mshandete amesema Tanesco ikilidanganya baraza kuwa wataweka umeme vijiji vyote hata vile vilivyokuwa vimeainishwa kuwa vitawekewa umeme mpaka sasa havijawekewa hali ambayo imekuwa ikizorotesha maendeleo ya halmashauri kwa sababu umeme ukiwepo na kipato cha halmashauri kitaongezeka.
 

Naye diwani wa kata ya Salawe Joseph John amesema Salawe kuna umeme lakini umekuwa ukikatika katika kila siku na kusababisha kuunguza vitu mbalimbali vinavyotumia umeme, hivyo aliomba lifanyiwe kazi kwa haraka ili watu wasiendelee kupata hasara pia transformer ziongezwe kwenye maeneo mbalimbali ya vijiji.


Akijibu hoja za madiwani Mhandisi mkuu wa Tanesco Kulwa Mangara amesema maeneo yote ambayo hayajawekewa umeme yatawekewa awamu kwa awamu na kule zilikoondolewa nguzo wataagiza zirudishwe, hivyo changamoto zote zilizopo zitafanyiwa kazi.

Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri hiyo Ngasa Mboje amesema katika suala la umeme usiwadanganye madiwani unahitajika utekelezaji mkubwa kwa sababu asilimia kubwa ya madiwani wamelalamikia changamoto ya umeme.

Naye mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasitha Mboneko amesema hakuna gharama iliyopandishwa katika umeme wa Rea bado ipo pale pale wasipindishe maelekezo ya serikali na kuongeza gharama bei ya Tanesco kwa maeneo ya vijijini ni sh 27,000.

"Pia niwaombe mnapopeleka nguzo pelekeni kwenye vijiji husika ili msiwachonganishe wananchi vijij vyote vinatakiwa vipate umeme na kweli kuna vijiji havina umeme kabisa pelekeni umeme pia muongeze transformer ili halmashauri ipate mapato"amesema Mboneko.

Hata hivyo meneja wa Tanesco alivyoongea na gazeti la Mwananchi kuhusiana na tuhuma hizo amesema " leo sio siku ya kazi lakini pia kwenye baraza hilo nilituma mwakilishi hivyo atanieleza ni vijiji gani vinalalamikiwa nitatoa majibu kwenye kikao cha baraza la madiwani kijacho.

Post a Comment

0 Comments