Header Ads Widget

FEDHA ZA CSR ZA BARRICK BULYANHULU ZAFANIKISHA MIRADI MIKUBWA YA SEKTA YA ELIMU NA AFYA WILAYANI NYANG’HWALE


Mwakilishi wa Mkuu wa wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita, Bi.Khadija Zegeja, (Katikati), akitoa ripoti kwa Maofisa waandamizi wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu waliotembelea miradi ya maendeleo iliyofanikishwa na fedha za kusaidia jamii zilizotolewa na mgodi huo (CSR) wilayani humo,kulia kwake ni Meneja Mkuu wa Barrick Bulyanhulu,Cheick Sangare na kushoto aliyevaa koti ni Kaimu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo,Bw, Leonard Bathromeo Mgema,wengine ni Maofisa wa Barrick Bulyanhulu na Halmashauri ya Nyang’hwale.
Maofisa Waandamizi wa Barrick Bulyanhulu wakielekea kutembelea maabara ya sekondari ya Nyigundu.
**

Wananchi wanaoishi wilayani Nyang’hwale mkoani Geita, wanaendelea kufurahia uwekezaji wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, kutokana na kuboreshewa miundo mbinu katika sekta ya elimu, afya na maji kupitia fedha za kusaidia huduma za kijamii (CSR) zinazotolewa na mgodi huo ambazo zimewezesha maisha yao kuendelea kuwa bora.

Baadhi ya miradi mikubwa iliyotekelezwa wilayani humo ni kujengwa kwa shule ya awali na msingi ya kisasa ya Kharumwa inayomilikiwa na Halmashauri ya Nyang’hwale, katika kitongoji cha Butalanda, inayofundisha masomo kwa mchepuo wa kingereza ambapo fedha za CSR zilizotolewa na Barrick Bulyanhulu kufanikisha mradi huo ni shilingi milioni 300.

Miradi mingine ambayo fedha za CSR zimechangia kuifanikisha ni ujenzi wa bwalo la chakula katika shule ya Sekondari ya Msalala, shilingi milioni 94,720,000/-,ukarabati wa madarasa 3,shilingi milioni 25,491,200/-,na ujenzi wa madarasa 2 katika sekondari ya Nyijundu kwa gharama ya shilingi milioni 20.

Pia fedha hizo zimefanikisha miradi ya ujenzi wa hosteli ya Wasichana katika shule ya sekondari ya Mwingiro,shilingi 115,858,200/-, ujenzi wa maabara ,shilingi milioni 100,ujenzi wa bwalo la chakula katika sekondari ya Nyang’hwale kwa gharama ya shilingi milioni 114,818,000/- na ukarabati wa vyumba 3 vya madarasa kwa shilingi milioni 18,043,200/-.

Miradi mingine ni ujenzi wa zahanati ya Lushimba kwa shilingi 70,676,275 na ujenzi wa nyumba ya watumishi katika zahanati hiyo kwa shilingi milioni 25,731,650. zahanati ya Lushimba ambayo itawaondolea wananchi adha ya kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kupata huduma za afya.

Akiongea kuhusiana na miradi hiyo inavyoendelea kuboresha maisha ya wananchi wakati wa ziara ya viongozi wa Barrick Bulyanhulu, walipotembelea miradi hiyo,Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Nyang’hwale,Bw, Leonard Bathromeo Mgema, alisema fedha za CSR zimeleta faraja kubwa kwa wananchi na kuwezesha maisha yao kuendelea kuwa bora.

“Kuwepo kwa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu Jirani na Wilaya yetu kumeipa heshima Wilaya yetu kwani kupitia fedha za CSR ambayo kwetu sisi tunayahesabu kama mapato ya ndani imetufanya kutekeleza miradi mingi ya Elimu, Afya na Maji na mingine mingi”,alisema Mgema.

Alisema ujenzi wa shule ya mchepuo wa kingereza kumeondoa adha ya watumishi na wafanyabiashara wa eneo hilo waliokuwa wanahangaika kuwapeleka watoto wao maeneo ya mbali kupata elimu pia jambo la kufurahisha shule nyinginezo za Serikali zimezidi kuimairishiwa miundo mbinu na kuwezesha watoto kuendelea kupata elimu katika mazingira rafiki.

Naye Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari ya Msalala, Bw. Mpuya Charahani, alitoa shukrani kwa uongozi wa halmashauri ya Nyang’hwale na mgodi wa Barrick Bulyanhulu kwa kuboresha miundo mbinu ya shule hiyo kupitia fedha za mfuko wa CSR.


Baadhi ya wananchi wanaoishi wilayani Nyang’hwale walieleza kuwa wanaendelea kufurahia uboreshwaji wa huduma mbalimbali za kijamii katika maeneo yao kutokana na fedha zinazotolewa na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, kupitia halmashauri ya wilaya hiyo.


Meneja Mkuu wa Mgodi wa Bulyanhulu, Bw.Cheick Sangare,jana akiambatana na ujumbe wa Maofisa Waandamizi wa Mgodi walitembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa fedha za kusaidia huduma za kijamii (CSR) zinazotolewa na Mgodi huo kwa Halmashauri ya Nyang’hwale.

Ujumbe huo wa Barrick Bulyanhulu, ulifurahishwa kuona jinsi miradi mbalimbali inavyoendelea kwendana na lengo lililokusudiwa la kuboresha maisha ya wananchi kupitia fedha zinazotolewa na Mgodi kwa ajili ya kufanikisha miradi ya kijamii.


Kwa Upande wake Meneja Mkuu wa Barrick, Cheick Sangare, amewakikishia wananchi wa Nyang’hwale, kwamba Mgodi wa Barrick, upo kwa ajili ya kuhakikisha jamii inanufaika na faida inayotokana na mauzo ya dhahabu pia alisema Mgodi utaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuchangia kuleta maendeleo kwa wananchi na aliahidi kuwa changamoto mbalimbali alizokutana nazo katika ziara hiyo zitafanyiwa kazi na kupatikana suluhisho.
Ujumbe wa Maofisa Waandamizi wa Barrick wakitembelea miundo mbinu ya shule ya Sekondari ya Nyigundu.
Sehemu ya madarasa yaliyojengwa katika shule ya sekondari ya Nyang'hwale
Mwonekano wa jengo la hosteli ya wasichana katika shule ya sekondari ya Mwigiro ambalo limejengwa kwa fedha za CSR zilizotolewa na Barrick Bulyanhulu.
Sehemu ya jengo la zahanati ya Lushimba,kampuni pia imewezesha ujenzi wa nyumba za kuishi wafanyakazi katika zahanati hiyo.
 

Post a Comment

0 Comments