Header Ads Widget

MGODI WA NORTH MARA WACHANGIA KUPUNGUZA MAAMBUKIZI YA UKIMWI KWA ZAIDI YA ASILIMIA 50


Daktari Mkuu wa Barrick North Mara, Dkt. Nicholaus Mboya akitoa ufafanuzi kwa wajumbe wa Kamati ya Bunge ya masuala ya UKIMWI
Meneja wa Mahusiano ya Kijamii wa Barrick North Mara,Gilbert Mworia akitoa maelezo kwa wajumbe wa Kamati ya Bunge ya masuala ya UKIMWI.
Mkuu wa wilaya ya Tarime,Kanali Michael Mntenjele akiongea wakati wa kikao hicho
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya bunge ya masuala ya UKIMWI wakifuatilia maelezo ya watendaji wa Barrick wakati wa ziara hiyo.


**

Tangu ianze kumiliki na kudhibiti uendeshaji wa mgodi wa dhahabu wa North Mara mnamo mwaka 2019, kampuni ya Barrick Gold Corporation (NYSE: GOLD) (TSX: ABX), imefanikiwa kupunguza kiwango cha maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa zaidi ya nusu miongoni mwa wafanyakazi wa mgodi na jamii zinazozunguka mgodi huo kutoka kiwango cha juu cha 3.3% mwaka 2018 hadi 1.5% mwaka jana.

Wakati huo, maambukizi mapya ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) yamepungua kutoka kiwango cha juu cha 16% mwaka 2018 hadi 10% mwaka 2021, wakati kiwango cha magonjwa yote ya zinaa yamepungua kutoka asilimia 4.78% mwaka 2017 hadi 2.95% mwaka 2021.


Akiwasilisha maboresho hayo kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge la Tanzania ya Masuala ya UKIMWI, iliyotembelea mgodi huo mwishoni mwa wiki kujadili hatua za kampuni za kupambana na magonjwa ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI (VVU) na Kifua Kikuu (TB), Meneja Mkuu wa mgodi wa North Mara, Apolinary Lyambiko, alisema mpango wa VVU/UKIMWI wa kampuni umejikita katika kuongeza uelewa, kuhimiza ngono salama na kuhimiza kupata Ushauri Nasaha na Upimaji wa Hiari (VCTs).

“Katika hili, Barrick ina sera pana kuhusiana na VVU/UKIMWI mahali pa kazi; ambayo Imekuwa ikitekelezwa kwa kushirikisha Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO) na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs), kwenye kampeni zake za kuhamasisha Upimaji wa Hiari (VCT) kusambaza kondomu za bure, kugawa vipeperushi vya kuelimisha na T-shirt, kutoa huduma za uchunguzi wa hali ya afya mara kwa mara; kuboresha mazingira kuhakikisha kuna hewa safi na kufuatilia hali ya usafi katika maeneo yake ya kazi ,” aliongeza.

Kwa upande wa jamii, Barrick imeanzisha kampeni mbalimbali za uhamasishaji kwa kushirikiana na Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO) ikiwemo maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani ya mwaka 2020 na 2021. Maadhimisho ya mwaka 2021 yalijumuisha kampeni kabambe ya wiki mbili ya uhamasishaji wa masuala mbalimbali ya afya. Aidha, katika kampeni hiyo zaidi ya watu 4,800 walifanya upimaji wa hiari wa afya zao,uniti 1,000 za damu zilikusanywa, Vifaa 1,800 vya kupima VVU kwa haraka vilitolewa: tohara 134 zilifanyika; watu 164 walifanyiwa uchunguzi wa saratani ya shingo ya kizazi; na maelfu ya kondomu, T-shirt, na vipeperushi vya uhamasishaji vilitolewa kwa wananchi.


Lyambiko aliendelea kusema kwamba “magonjwa kama vile Kifua Kikuu na UKIMWI yanakwamisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya maeneo yanayozunguka mgodi na kuweza kuathiri shughuli zake. Jitihada za kupunguza na kuondoa magonjwa haya katika jamii zetu sio tu sehemu muhimu ya kufanikisha mkakati wetu wa afya ya jamii bali pia kuleta faida katika biashara,” alisema.

Post a Comment

0 Comments