Header Ads Widget

RC MJEMA AFANYA ZIARA WILAYANI KISHAPU AWATAKA WANANCHI KUTUNZA MIUNDOMBINU YA BARABARA NA MADARAJA

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, akizungumza kwenye ukaguzi wa ujenzi wa miundombinu ya Madaraja wilayani Kishapu.

Na Marco Maduhu, KISHAPU

MKUU wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, amewataka wananchi mkoani humo, kuitunza miundombinu ya barabara pamoja na madaraja, ili idumu kwa muda mrefu kuwahudumia na kuitumia katika shughuli za kiuchumi ikiwamo kusafirisha mazao.


Mjema amebainisha hayo leo alipokuwa wilayani Kishapu kukagua ujenzi wa miundombinu ya madaraja mawili makubwa, ambayo yamejengwa Ukenyenge na Itilima wilayani humo, kwa fedha za Tozo za mafuta ya Petrol na Diesel.

Alisema Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwamo miundombinu ya Barabara, Makalavati, na Madaraja, na kuwataka wananchi wote mkoani humo kuitunza miundombinu hiyo ili idumu kwa muda mrefu.

“Ujenzi wa daraja hili na Ukenyege limegharimu kiasi Sh.bilioni 1.5 na daraja la Ipeja-Itilima Sh.milioni 486 fedha ambazo zinatokana na Tozo za Mafuta ya Petrol na Diesel, pongezi sana kwa Rais wetu Samia Suluhu Hassani kwa kutupatia fedha hizi Shinyanga, na sasa zinatekeleza miradi mikubwa kwa wananchi,”alisema Mjema.

“Naombeni sana wananchi muitunze miundombinu ya Barabara na Madaraja, pamoja na kutoharibu alama za usalama barabarani, ili Serikali tusiingie gharama za kutenga fedha za mara kwa mara kwa ajili ya kuzifanyie matengenezo, ili fedha hizo zikatekeleze miradi mingine ya maendeleo,”aliongeza.

Pia aliwataka Wakandarasi ambao wanatekeleza miundombinu hiyo ya Madaraja waitekeleze kwa kiwango kinachotakiwa na thamani ya fedha ionekane, pamoja na kuikamilisha kwa wakati ili wananchi waanze kuitumia.

Katika hatua nyingine, amewaagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoani Shinyanga, kudhibiti Magari yenye uzito mkubwa kutopita kwenye Barabara na Madaraja hayo ili kutoharibu miundombinu hiyo.

Kwa upande wake kaimu Meneja wa TANROADS Mkoani wa Shinyanga Mhandisi Jessica Manang, alisema Magari ambayo yanaruhusiwa kupita kwenye Barabara na Madaraja ni yale yasiyozidi Tani 50, huku akiahidi kulifanyia kazi agizo hilo la kudhibiti Magari yenye uzito mkubwa kupita kwenye miundombinu hiyo.

Naye Diwani wa Ukenyenge Anderson Mandia, alisema ujenzi wa daraja kubwa katika eneo hilo litakuwa msaada mkubwa kwa wananchi, ambapo wataepukana na ajali za mara kwa mara, pamoja na kulitumia kufanya shughuli zao za kiuchumi, sababu daraja mama ni finyu na halina usalama.

Nao baadhi ya Wananchi wa Kishapu kwa Nyakati tofauti walisema, ujenzi wa miundombinu hiyo ya Barabara na Madaraja mawili makubwa ya Ukenyenge na Itilima, yatawasaidia sana katika shughuli zao za kiuchumi, hasa wakati wa kusafirisha mazao, na kuahidi kushirikiana na Serikali kuilinda miundombinu hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, akizungumza kwenye ukaguzi wa ujenzi wa miundombinu ya Madaraja wilayani Kishapu.

Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kishapu Shija Ntelezu, akizungumza kwenye ziara hiyo ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya Madaraja.

Diwani wa Ukenyenge wilayani Kishapu Anderson Mandia, akizungumza umuhimu wa ujenzi wa daraja kubwa kwenye Kata hiyo, wakati wa Ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya Madaraja wilayani humo.

Kaimu Meneja TANROADS Mkoani wa Shinyanga Mhandisi Jessica Manang, akitoa taarifa za utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya ujenzi wa daraja la Ukenyenge wilayani Kishapu.

Meneja TARURA wilayani Kishapu Wilfred Guta, akitoa taarifa za ujenzi wa miundombinu ya daraja la Ipeja-Itilima wilayani humo.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, (katikati) akikagua akikagua ujenzi wa miundombinu ya daraja la Ukenyenge wilayani Kishapu.

Muonekano wa daraja la Ukenyenge wilayani Kishapu.

Muonekano wa daraja la Ipeja-Itilima wilayani Kishapu.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, akizungumza na Wanawake wa Ukenyenge wilayani Kishapu, ambao wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassani, kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, akiwa ziara wilayani Kishapu ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya Madaraja.


Na Marco Maduhu, KISHAPU.














Post a Comment

0 Comments