Header Ads Widget

JPM: SINA AHADI ZA UONGO, NAPENDA NIFIKE MBINGUNI


Mgombea Urais kupitia CCM, Dkt John Pombe Magufuli.

Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM Dkt John Magufuli, amesema kuwa yeye hatoa ahadi za uongo kwa sababu hataki kufanya dhambi hiyo kwani anatamani siku moja akienda mbinguni apewe Uwaziri wa Malaika.

  Kauli hiyo ameitoa hii leo Septemba 2, 2020, katika eneo la Misigiri mkoani Singida wakati akiomba kura kwa wananchi wa maeneo hayo.

"Mimi sitoi ahadi za uongo kwa sababu msema kweli ni mpenzi wa Mungu, sitaki nifanye dhambi kwa kuwaambia wazee wangu ya uongo, ninapenda na mimi siku moja nifike mbinguni ili Malaika nikifika waniambie ulifanya vizuri tunakupa sasa hata ka Uwaziri wa Malaika", amesema Dkt Magufuli.

Katika hatua nyingine Dkt Magufuli ameeleza ni kwa namna gani anawapenda Mwigulu Nchemba ambaye ni Waziri wa Katiba na Sheria na Mgombea Ubunge wa Jimbo la Ubungo, Profesa Kitila Mkumbo.

"Mwigulu ninamfahamu na ninampenda sana, lakini Mwigulu ni kama mdogo wangu maana amesoma Chuo Kikuu na mdogo wangu na Profesa Mkumbo ni mdogo wangu naye nampenda sana, ndiyo maana nikasema huyu agombee hapa na yule akagombee Ubungo na watashinda na mimi najua nitafanya nini", ameongeza Dkt Magufuli.