` AMANI NGUZO YA KILIMO: WAKULIMA WA PAMBA WASISITIZA KULINDWA KWA TUNU ZA TAIFA

WANDAMAN HOTEL

AMANI NGUZO YA KILIMO: WAKULIMA WA PAMBA WASISITIZA KULINDWA KWA TUNU ZA TAIFA

Wakulima wa pamba mkoa wa Shinyanga  na Simiyu wameeleza kuwa amani ni msingi muhimu unaowawezesha kuendesha shughuli zao za kilimo kwa ufanisi na mafanikio bila kusumbuliwa.

Wamesema bila uwepo wa amani ni vigumu kwa mkulima kufanya kazi zake kwa utulivu na kupata matokeo chanya,jambo ambalo linatakiwa kusimamiwa kwa nguvu zote.

Mohamedi Matani mkulima wa pamba kutoka Mkoa wa Simiyu amesema hali ya utulivu iliyopo kwa sasa imechangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa shughuli za kilimo, hususan uzalishaji wa zao la pamba.

Amesema  wanafanya kazi zao kwa bidii wakiamini kuwa mazingira salama ni kichocheo kikubwa cha maendeleo yao na kuwa na uhakika wa kipato na chakula kwenye familia.

Said Tangawizi ambaye ni mkulima wa Shinyanga amesema  amani inawawezesha sio tu kulima bali pia kuvuna na kusafirisha mazao yao bila hofu ya usalama wao wala mali zao. Hali hiyo imeongeza ari ya uzalishaji na kuimarisha uchumi wa wakulima .

Katika kusisitiza umuhimu wa amani, wakulima hao wamekumbushia tukio la Oktoba 29, 2025 wamesema lilisababisha taharuki na athari kubwa kwa jamii hawatamani kuona wala kusikia tena hali kama hiyo ikijirudia.

Wamesema tukio hilo linapaswa kuwa funzo kwa kila Mtanzania juu ya thamani ya amani, wakieleza kuwa ni rahisi kupotea lakini ni vigumu kurejeshwa,

Pamoja na hayo, wamewataka watanzania  kuendelea kuilinda amani kwa nguvu zote, wakisisitiza kuwa hakuna mahali pengine pa kwenda kutafuta amani endapo itapotea ni jukumu la kila mmoja kulinda tunu hiyo muhimu.

Amesema inawawezesha kufanya kilimo na kupata chakula cha uhakika kwani bila chakula cha kutosha, uchumi wa familia na taifa kwa ujumla unaweza kuyumba kwa kiasi kikubwa. 

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464