Header Ads Widget

CCM SHINYANGA YATISHIA KUFUTA MAJINA YOTE YA WAGOMBEA, RUSHWA YATAJWA


Katibu wa CCM mkoa wa Shinyanga, Donard Magesa

Suzy Luhende -Shinyanga

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Shinyanga, Donard Magesa amewaonya wagombea wa Jimbo la Shinyanga mjini kuacha kutoa Rushwa kwa wajumbe wanaopiga kura.

Onyo hilo amelitoa leo baada ya kupigiwa simu na Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dk. Bashiru Ally, ambapo amelazimika kukutana na wagombea wote wa chama hicho waliochukua fomu ili kuwapa onyo, maelekezo na taratibu zingine za chama wakati wakisubiri hatua zinazofuata baada ya zoezi hilo.

Magesa amesema vurugu wanayoifanya kwa sasa wagombea haifai kwani sio demokrasia hivyo amewaomba watulie wasubiri kwa amani mchakato wa kupigiwa kura za maoni.

"Ole wao watakaotusaliti katika uchaguzi huu, tutakula sahani moja, najua wapo na ninatangaza rasmi kuwa ni marufuku mgombea kutoa rushwa na atakayebainika tutamshughulikia, hivyo nakemea pepo la rushwa na mkiendelea kutoa rushwa tutafuta uchaguzi huu.


"Tuache kutembea nyumba kwa nyumba mkiendelea hivyo tutatangaza watu wengine wagombee upya, hivyo tukubaliane kuanzia leo acheni kutoa rushwa na tukubaliane kabisa atakayepatikana anatoa rushwa tumuweke ndani," amesema Magesa.

Hata hivyo, Magesa amewatoa wasiwasi wagombea hao juu ya tetesi za baadhi ya watia nia kutumwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli, ambapo amesisitiza kwa kusemakuwa "hakuna mtu aliyetumwa angekuwa ametuma mtu tungekuwa tumeshajua hayo ni maneno ya watu tu,".


Pia Katibu Magesa amewataka kamati ya siasa secretarieti ya wilaya kusimamia wagombea wasiendelee kufanya fujo ya kutoa rushwa wasipodhibiti kila mmoja atawapa barua ya kusimamishwa.

Mmoja wa wagombea, Dk. Kulwa Meshack ameomba msamaha kwa yale yaliyotokea hivyo ni vizuri yasiendelee lakini pia hata kama akishindwa atakuwa ni mmoja wa makampeni meneja watakaopangwa kutoka CCM.

Baadhi ya watia nia waliochukua fomu za kuomba kugombea ubunge jimbo la Shinyanga Mjini kwa tiketi ya CCM wakimsikiliza katibu wa chama hicho.