` JUKUMU LA MAJI SI LA SERIKALI TU; WANANCHI LAZIMA WAWE 'WALINZI NAMBA MOJA' WA VYANZO

JUKUMU LA MAJI SI LA SERIKALI TU; WANANCHI LAZIMA WAWE 'WALINZI NAMBA MOJA' WA VYANZO


Wito umetolewa kwa Watanzania kubadilisha fikra zao kuhusu upatikanaji wa maji, huku wakisisitizwa kuwa uwajibikaji wa uhifadhi wa rasilimali hii muhimu si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kitaifa, kisheria, na kimaadili kwa kila raia.

Wachambuzi wa ustawi  wanasema ili Tanzania ifikie Dira yake ya Uchumi wa Viwanda ya 2050, wananchi lazima wajione kama 'Walinzi Namba Moja' wa Rasilimali Maji, wakikubali ukweli wa gharama halisi za maji safi na kulinda vyanzo kwa ukali.

Dhana potofu ya kwamba maji yanapaswa kuwa bure au kugharimu kidogo ndiyo inaathiri uwezo wa mashirika ya maji kufanya matengenezo. Inasisitizwa kuwa maji hugharimu sana katika kusukuma, kutibu kwa kemikali, na kusambazwa kwa umeme mwingi kutoka vyanzo vya mbali kama Mto Ruvu.

Kama wananchi hawalipii gharama halisi, mashirika hukosa mapato ya kutosha kufanya ukarabati na kupunguza maji yasiyoingiza mapato (NRW), na hivyo kuhujumu moja kwa moja uwezo wa Serikali kutoa huduma ya uhakika.

Aidha wananchi wananchi wanaoishi karibu na vyanzo vya maji ndio vikosi vya ulinzi vya kwanza. Badala ya kuacha lawama kwa Serikali pekee, jamii zinapaswa kufanya ufuatiliaji wa kijamii kwa ukali zaidi kuona kwamba hakuna uharibifu unaofanyika kwenye chanzo au njia ya maji yaani mto.

" Kila mti uliokatwa katika maeneo ya vyanzo huondoa uwezo wa asili wa ardhi kunyonya mvua. Mtu yeyote anayefanya uharibifu—kama kukata miti au kilimo kiholela katika maeneo oevu—anapaswa kuonekana kama mhalifu wa kiuchumi na kuripotiwa mara moja," anasema mmoja wa wachambuzi hao Said Mmanga.

Katika maeneo kama Dar es Salaam, wananchi wanatakiwa kuripoti uchimbaji wa visima bila kibali ili kuepusha hatari ya Kuingia kwa Maji ya Chumvi (Saline Intrusion), ambayo inaweza kuharibu kabisa maji ya ardhini.

Kutokana na mabadiliko ya tabianchi, baadhi ya wataalamu wanashauri nchi kuanza kufikiria kusafisha maji ya bahari (Desalination). Ingawa teknolojia hii ni ghali sana, inatoa uhakika wa maji kwa asilimia 100 dhidi ya ukame, hasa kwa jiji la biashara linalolenga Dira ya 2050. Wananchi wanapaswa kuijiandaa kisaikolojia kukubali ongezeko la gharama kwa ajili ya usalama wa maji.

 Ulinzi wa maji unahitaji mabadiliko ya utamaduni wa jamii. Kila Mtanzania, awe anaripoti uvujaji wa bomba au anapanda mti, ni mwekezaji muhimu katika sekta ya maji, na hivyo kuhakikisha vizazi vijavyo na viwanda vinapata maji ya kutosha kufikia malengo ya kitaifa.

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464