` TAASISI ZA ELIMU ZASHAURIWA KUTOA ELIMU KUHUSU DIRA YA TAIFA 2050

TAASISI ZA ELIMU ZASHAURIWA KUTOA ELIMU KUHUSU DIRA YA TAIFA 2050

 

Wakili msomi Ipilinga  Panya ambaye ni mgeni rasmi mahafali ya 32 ya shule ya sekondari uhuru-manispaa ya Shinyanga.

Mkuu wa shule ya sekondari  uhuru sekondari ,Mwalimu Victoria  Nakuyaumu akizungumza katika mahafali ya 32 ya shule hiyo.

TAASISI ZA ELIMU ZASHAURIWA KUTOA ELIMU KUHUSU DIRA YA TAIFA 2050

NA EUNICE KANUMBA 

Taasisi za elimu nchini zimeshauriwa kuanza mchakato wa kutoa elimu kuhusu Dira ya Taifa ya 2050 ili kusaidia maandalizi ya rasilimali watu watakaoweza kukabiliana na mabadiliko ya kijamii na kiuchumi katika miaka ijayo.

Wito huo umetolewa oktoba 17,2025 na Wakili msomi Ipilinga  Panya, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 32 ya Shule ya Sekondari Uhuru iliyopo katika Manispaa ya Shinyanga ambapo wakili huyo katika safari yake ya elimu alisoma katika shule hiyo kwa elimu ya kati

Wakili Panya amesema   ni muhimu taasisi za elimu kuanza mapema kufundisha wanafunzi kuhusu dira hiyo, kwani ndani ya miaka 25 ijayo kundi la vijana waliopo mashuleni ndilo litakuwa na jukumu kubwa la kuleta maendeleo ya Taifa.

“Shule ya Sekondari Uhuru iwe mfano wa kwanza nchini kuanzisha somo au mafunzo kuhusu Dira ya Taifa ya 2050, ili kuepusha kizazi kijacho kuingia kwenye changamoto bila maandalizi, kana kwamba kinaelea mtoni huku mikono na miguu vikiwa vimefungwa kamba,” amesema wakili  Panya.

Aidha akizungumzia mapambano dhidi ya rushwa wakili Panya amesema  kuwa  ni muhimu elimu dhidi ya rushwa pia ikatiliwe mkazo mashuleni, ili kujenga misingi ya haki, uwajibikaji na maendeleo endelevu katika jamii.

Katika kuchangia maendeleo ya shule hiyo, Wakili Panya ametoa  mashine mbili za kunakilia (photocopy) pamoja na fedha taslimu kiasi cha shilingi  milioni moja  kwa ajili ya ujenzi wa jiko la shule,ambalo lipo mbioni kukamilika.

Akitoa shukrani, Afisa Elimu wa Sekondari -Manispaa ya Shinyanga, John Musa, amesema  mgeni rasmi ni zao halisi la shule hiyo na amejitokeza kwa moyo wa kizalendo kusaidia uboreshaji wa miundombinu ya shule hiyo ikiwemo jiko la kupikia  kama sehemu ya mchango wake katika sekta ya elimu ya manispaa ya Shinyanga.

“Serikali itachukua hatua kukamilisha sehemu iliyosalia, lakini tunatoa wito kwa watu wengine wenye nafasi kama hizi kuunga mkono shule walizosoma ili kuongeza ubora wa elimu,” amesema  Musa.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Afisa Elimu  ya watu wazima  Manispaa ya Shinyanga  Betrice Mbonea, alitoa wito kwa jamii kuhamasisha watoto wao kuendelea na masomo hata kama walisitisha   kutokana na changamoto mbalimbali kama vile  mimba za utotoni au hali duni ya uchumi na kuanisha kuwa   serikali imeweka utaratibu wa elimu mbadala kwa wanafunzi waliokatishwa masomo ili kuhakikisha hakuna anayekosa fursa ya elimu.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Sekondari Uhuru, Kanali Mstaafu John Kayoka, amewasihi  wazazi na walezi kuendeleza jukumu la kuwasimamia watoto wao ili kuwaepusha na mwenendo usiofaa.

“Wanafunzi wanapaswa kujitunza na kufuata maadili mema ili wasizimishe ndoto zao, kwani wao ndiyo viongozi wa baadaye wa Taifa,” amesema  Kanali Kayoka.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule hiyo, Mwalimu Victoria  Nakuyaumu, amesema  shule  hiyo imekuwa ikifanya vizuri kitaaluma kila mwaka, ambapo kwa mwaka 2025 imefanikiwa kufikisha wastani wa asilimia 75 ya wanafunzi wanaoendelea kidato cha tano.

“Mwaka huu tunawahitimu wanafunzi 226, kati yao wasichana 113 na wavulana 113, na tunatarajia matokeo mazuri kutokana na nidhamu na juhudi kubwa za walimu,” amesema  Nakuyaumu.

Shule ya Sekondari Uhuru imeanzishwa mwaka 1990  ikiwa na mikondo miwili tu na hadi sasa (mwaka 2025) ina jumla ya wanafunzi 1,020. Wanaosoma katika shule hiyo.

MWISHO

Kama una Taarifa, Habari, Tangazo n.k Wasiliana nasi kupitia shinyapress@gmail.com au +255 788 469 464