Header Ads Widget

SABABU WAZAZI KUKWEPA KUWAPELEKA WATOTO KLINIKI ZABAINIKA

SABABU ZA WAZAZI KUKWEPA KUWAPELEKA WATOTO KLINIKI ZABAINIKA

Na Tonny Alphonce,MWANZA

Imebainika kuwa wazazi wengi wenye watoto wenye umri wa miaka 2 – 3 huacha kuendelea kuwapeleka watoto wao Kliniki na kuwasababishia magonjwa mbalimbali yanayoweza kuathiri ukuaji wao.

Ukizungumza na baadhi ya wazazi hawa utagundua sababu mbalimbali zinazopelekea wao kuacha kuwapeleka watoto wao Kliniki ili waweze kupatiwa chanjo za aina mbalimbali pamoja na kuangaliwa maendeleo ya afya zao katika ukuaji wao wa kila siku.

Baadhi ya wazazi wametaja sababu hizo kuwa ni kukosekana kwa huduma za afya katika maeneo wanayoishi,kutopata elimu juu ya umuhimu wa kumpeleka mtoto Kliniki pamoja na wazazi kutumia muda mwingi katika shughuli za kiuchumi.

Mariam Tandu mkazi wa kata ya Luchelele mtaa wa Ngaza mkoani Mwanza anasema sababu kubwa iliyomfanya kuacha kumpeleka mtoto wake Kliniki tangu alipokuwa na umri wa miaka 2 ni kutokana na umbali uliopo kutoka eneo analoishi hadi kwenye Zahanati ya Shadi.

“Kusema kweli mimi niacha kumpeleka Kliniki kwa sababu ni mbali ni kama kilometa 6 sasa nilimwangalia mtoto nikaona anaendelea vizuri haumwi nikaacha hadi leo ndio kaanza kupata huduma ya chanjo baada ya wataalamu hawa wa afya kuja kwenye kituo chetu hiki cha kulelea watoto,tunalishukuru sana hili shirika la Dunia Rafiki wanawasaidia sana watoto wetu hapa Ngaza”.alisema Mariam.

Nae Joseph Elisha mkazi wa mtaa wa Ngaza amesema kuwepo kwa kituo hicho cha malezi katika mtaa wao ni neema kubwa kwa kuwa watoto wanalelewa katika mazingira salama lakini wanapata nafasi nzuri ya kupata huduma za afya pamoja na ufatiliwaji wa ukuaji mtoto.

“Huu upimaji wa uzito,dawa za minyoo wanazopatiwa watoto ni jambo zuri hii itanisaidia pia mimi mzazi kuangalia lishe nayompa mtoto maana nikipata taarifa mtoto wangu kapungua uzito tajulishwa na mimi tajiangalia niongeze nini kwenye lishe ya mwanangu”.alisema Elisha

Mkurugenzi wa Kituo hicho cha Kijamii Cha Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto Sophia Asenga, amesema wameamua kushirikiana na Zahanati ya Shadi kutoa huduma ya dawa za Minyoo,Matone ya Vitamin A na Upimaji uzito kwa watoto baada ya kugundua watoto wengi waliopo mtaa wa Ngaza hawapati huduma ya Kliniki.

Sophia amesema wameendesha huduma hiyo ya upimaji kwa watoto zaidi ya 30 waliopo katika kituo hicho na wengine wa nje ya kituo hicho kwasababu ni muhimu katika ukuaji wao lakini inasaidia kujua pia maendeleo ya ukuaji wa mtoto na endapo atapata tatizo lolote ni wazi kuwa wahuduma wa afya watagundua mapema na kumaptia matibabu sahihi.

“Mtaalamu wetu wa afya kupitia zoezi hili la leo ameona afya za watoto wetu hapa mtaani Ngaza na wengine amegundua baadhi ya watoto wanachangamoto ya ugonjwa wa ngozi na tayari tumewapa taarifa wazazi ili wawapeleke hospitali kupatiwa tiba”.alisema Sophia.

Nae muuguzi wa Zahanati ya Shadi Maria Geoffrey amewataka wazazi kuendelea kuwapeleka Kliniki watoto hadi wanapofikisha umri wa miaka mitano kwani ni kipindi ambacho wataalam wanaendelea kufuatilia afya ya mtoto ili kumwezesha kufikia ukuaji timilifu.
Muuguzi wa Zahanati ya Shadi Maria Geoffrey akimpima mmoja wa watoto waliofika katika kituo cha Malezi.

Maria amesema wazazi wengi wanafanya makosa kuacha kuwapeleka watoto Kliniki hasa watoto wenye umri wa miaka 2-3 kwasababu bado wanatakiwa kupatiwa chanjo hizi za matone, Vitamin A na dawa za minyoo ambazo huwasaidia kujikinga na minyoo na vitamin A humkinga mtoto na maambukizi ya magonjwa ya macho.
Maria ameyataja magonjwa mengine yanayoweza kumpata mtoto asiyepata chanjo kuwa ni pamoja na kifua kikuu,ugonjwa polio, ugonjwa wa kuharisha,homa ya uti wa mgongo, pepo punda, kifaduro, surua,homa ya ini, vichomi lakini pia mtoto anaweza kupoteza maisha.

Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Mwanza Faithmary Lukindo amesema mkoa wa Mwanza umekuwa ukitumia njia mbalimbali kuhakikisha watoto wote walio katika umri wa kupatiwa chanjo wanachanjwa kupitia huduma ya mkoba ambayo huwafayta wananchi walipo.

FAITHMARY LUKINDO
Faithmary amesema mkoa pia umekuwa ukiendesha kampeni mbalimbali za chanjo na kutolea mfano kampeni iliyofanyika mwaka huu tarehe 15 hadi 18 mwezi wa pili iliitwa '' Onyesha upendo, Mpeleke Mtoto akapate chanjo'' ambapo matarajio ilikuwa kuwachanja watoto 81,449 watachanjwa na jumla ya dozi 85,520 za chanjo za surua na rubella zimepokelewa katika wilaya ya Nyamagana.

“Tunajua baadhi ya wazazi wamekuwa hawawapeleki watoto kliniki na ndio maana kwenye kampeni hii tuliyofanya mwezi wa pili wahusika wa chanjo hii walikuwa watoto kuanzia miezi 9 hadi miaka 4 na miezi 11 bila kujali chanjo walokwisha kupewa mwanzo kwa kuwa haina madhara bali inaongeza nguvu na kumfanya mtoto awe na kinga imara”.alisema Faithmarry

Mpango wa Taifa wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali unaonyesha kundi la umri wa miaka 3-5 linatakiwa kuendelea kupata huduma nyingine za lishe kama vile ufuatiliaji wa ukuaji, nyongeza ya vitamini A, vidonge vya minyoo na usimamizi jumuishi wa magonjwa ya watoto.
Hata hivyo inaonyesha pia changamoto iliyobaki ni wazazi kuacha kupeleka watoto wao kwenye kliniki za RCH mara kwa mara baada ya kumaliza chanjo wafikapo miaka 2.

Post a Comment

0 Comments