Header Ads Widget

BIBI APIGA MAGOTI KWA MWALIMU KUMUOMBEA MJUKUU WAKE ASIRUDIE DARASA


Bibi akiwa na mjukuu wake  baada ya kufika ofisi ya mwalimu mkuu akimuombea asirudie darasa.

Na  Kareny  Masasy,

MWANAFUNZI wa darasa la nne shule ya msingi Lyabukande Sara Shija (13) amejikuta akibubujikwa na machozi mbele ya mwalimu mkuu  wa shule hiyo akikataa kurudia.

Machozi yake yalikuwa yakimaanisha hataki kuendelea na shule kutokana na kurudia darasa la nne kwa mara ya tatu mfululizo.

Shija anaonekana kuongozana na bibi yake  ambaye anamlea nakuja moja kwa moja kwenye ofisi ya mwalimu mkuu.

Shija anasema  hataki shule kwani hajui kusoma wala kuandika mpaka sasa licha  ya kurudia darasa hilo kwa mara ya tatu sasa.

Bibi yake  anayefahamika kwa jina la  Nyasoro Sengerema (69) anaanza kujieleza kwa mwalimu ujio wake na mwanafunzi huyo (mwijukuu).

Sengerema anasema  amemleta  Sara Shija ambaye matokeo ya darasa la nne yalivyotoka nakusikia amefeli amekataa kuja shule.

Sengerema  ambaye hajui kusoma wala kuandika  anapiga magoti mbele ya mwalimu mkuu kutaka mwijukuu wake aendelee na darasa la Tano.


‘Mwalimu nimekuja mwanafunzi amekataa kuja tena shule baada ya kuona  anarudia rudia darasa  nimekuja kukuomba muacheni aendelee na darasa la Tano”anasema  Sengerema.

Sengerema anasema  mwanafunzi huyo amekuwa akitoka nyumbani   nakuhudhuria masomo shuleni kila siku sio mtoro.

Sengerema anaulizwa na mkuu wa shule  kazi za nyumbani huwa zinafanywa na nani hasa? anajibu  huwa anazifanya mwanafunzi huyo kutokana na mama yake kuwa ni mgonjwa wa akili.

Mjomba wa mwanafunzi huyo Juliaus Samweli anasema  hakujua kama  amefeli mara tatu alijua yuko darasa la sita.

“Leo ndio najua  amefeli na yuko darasa la nne lakini hajui kusoma wala kuandika hilo anafahamu pia anautoro wa rejareja”anasema Samweli.

Samweli anatoa ushauri kwa mtoto wake huyo arudie kwani akikaa nyumbani  itakuwa rahisi kurubuniwa nakupata mimba za utotoni.

“Serikali iangalie mazingira ya vijijini ni tofauti na mjini wawape fursa  wa vijijini wanapofeli waendelee na  darasa lingine kwani huenda mazingira ndiyo yanayosababisha tofauti na mjini”anasema Samweli..

Mwenyekiti wa kijiji cha Lyabukande  Peter Labacha anasema zamani wazazi walikuwa na desturi ya kuwaeleza watoto wao wafanye vibaya mitihani ili wakishindwa wawaozeshe.

“Wanaenda wanabadilika kidogokidogo kwa elimu inayoendelea kutolewa na mashirika yanayopinga vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto”anasema  Labacha.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Lyabukande   Jeremiah  Mashaka anasema   shule hiyo ilianzishwa mwaka 1956  imekuwa ikijitahidi kufanya vizuri  darasa la nne baadhi ya miaka.

Mashaka  anasema mwanafunzi huyo anamfahamu kwa mahudhurio darasani na ufaulu wake  ni kweli amerudia kutokana na kufeli mtihani wa darasa la nne.

Mashaka anasema  kurudia kwake ni mara ya tatu sasa kwani alioanza nao darasa la  kwanza wako darasa la sita mwaka huu.

 Mashaka anamjibu  bibi kuwa hawezi kwenda kinyume na  sera ya elimu  ya kwaka 2014 iliyofanyiwa maboresho mwaka 2016  kuwa mwanafunzi akifeli hawezi kuendelea na darasa lingine.

 “Historia ya mtoto huyu sikujua kama anaishi na bibi yake nilijua anaishi na wazazi wake amekuwa na utoro wa rejareja kila mwaka”anasema mwalimu  Mashaka.

  Mashaka anasema wazazi wa kata hii waliowengi wanawatumikisha watoto wa kike ndiyo walezi wa familia nakushindwa kumudu masomo.

 Mashaka anasema wanafunzi wa darasa la nne waliosajiliwa kufanya mtihani walikuwa 187 na waliofanya mtihani ni 182 wanafunzi watano hawakufanya mtihani kutokana na utoro.

Mashaka anasema wanafunzi 108 wamefaulu lakini  wanafunzi 74 wamefeli  kwa mwaka 2022  kati yao wasichana 46 na wavulana ni 28.

Mashaka anasema  shule nzima inawanafunzi 1002  na darasa moja linawanafunzi  zaidi ya 100 na Mwaka 2021 waliofeli  darasa la nne ni wanafunzi 69  wote wakarudia.

Mashaka anasema  zaidi ya wanafunzi 10  wengi wakiwa wasichana ndiyo wamerudia mara tatu mfululizo na ukifuatilia zaidi utakuta  wanalelewa na mzazi mmoja.

Mwalimu anayefundisha  darasa la nne  Herman  Shana anasema mwanafunzi Sara Shija ni mtoro wa rejareja  kati ya watoto  ambao walipangiwa kufundishwa na wanafunzi wenzao naye ni mmoja wapo.

“Tulifanya hivyo ili kuweza kumsaidia afaulu  wengine wamefaulu  kwani waliokuwa wamependekezwa kuwakumbusha pale waliposahau”anasema Mwalimu Shana.

Mratibu elimu kata  ya Lyabukande  Haruni Ibrahimu anasema  changamoto iliyopo watoto wengi wamefeli darasa la nne.

“Kufeli huko kumetokana  na utoro wa rejareja,kukabidhiwa  kulea familia  na wazazi kuwataka  wasaidiwe kazi za mashambani  na hawana muda wa kujisomea”anasema Ibrahimu.

Ibrahimu anasema  wazazi wamekuwa hawafuatilii  taarifa za watoto wao wanasubiri  wapate taarifa kutoka kwa walimu.

Mtendaji wa kata  hiyo Shadrack Malando anasema jamii inayoishi kwenye kata hii ni wakulima na wafugaji hivyo hawapendi watoto wao wasome.

Meneja mradi Sabrina Majikata  kutoka Shirika la Invest Childern Soceirty( ICS) lililopo mkoani Shinyanga lenye mradi uliolenga  kuwapati elimu  walimu juu ya   kuwatambua  wanafunzi mazingira wanayotoka ikiwa itasaidia kuwapa mbinu zaidi ya ufaulu.

Sera ya elimu ya mwaka 2014 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2016 imeeleza mwanafunzi atakaye feli mtihani wa darasa la nne ataruhusiwa kurudia.

Post a Comment

0 Comments