Header Ads Widget

MSIMU WA MAVUNO KILA MZAZI KUCHANGIA DEBE LA MAHINDI SHULENI






Wanafunzi wa darasa la awali shule ya msingi Puni

Na Kareny  Masasy Shinyanga

WAZAZI wa kijiji cha Puni halmashauri ya wilaya ya Shinyanga  wamedai msimu wa mavuno wako tayari kuchangia chakula shuleni bila wasiwasi wowote.

Wakazi wa kijiji hicho Somson Jeremiah na Suzana Gawinde wanasema  kwa mara ya kwanza walipewa Elimu juu ya faida ya wanafunzi kupata chakula shuleni mwaka 2019 kutoka shirika la kimataifa la Save the Children.

Jeremiah anasema shirika hilo lilihamasisha wazazi wa shule ya msingi Puni hasa kwa wanafunzi wa darasa la awali na kwanza kupata angalau uji nyakati za asubuhi.

“Tulishiriki ndani ya mwaka mmoja  kuchangia upatikanaji wa uji  kwa wanafunzi na badaye  ikasitishwa  ghafla lakini tungetekeleza ingezoeleka kwa wazazi sasa wanakumbushwa walishasahau”.anasema Jeremiah.

Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Puni  Leonard  Kawili anasema shule hiyo ilianzishwa mwaka 1976  ina wanafunzi 610  ambapo  darasa la awali wako  69 na darasa la kwanza wako  93.

“Mwaka 2019 wazazi  walihamasishwa kuchangia chakula shuleni lakini walianzia na unywaji uji kwa darasa la  awali na kwanza ili waweze kucheza na kusikia vizuri darasani”.anasema Kawili.

Mwalimu Kawili anasema sasa hivi hawapati chakula  shuleni ila wazazi walitoa ahadi kipindi cha Mavuno wako tayari kuchagia Mahindi ili kusaga nakupata unga wa uji.

Mwalimu  Kawili anasema Siku moja mtoto wa darasa la kwanza alikutwa amelala njiani hana nguvu  mwalimu alipofuatilia hadi kwa wazazi wake ikabainika anatoka kwenye familia duni na hakula usiku chakula chochote nyumbani.

Mwalimu Kawili anasema upatikanaji wa chakula shuleni unasaidia hata kwa watoto wanaotoka kwenye familia duni  kupata chakula na kupenda shule  kuondoakana na utoro wa rejareja.

Katibu wa jeshi la sungusungu  kutoka kijiji cha Puni  Abel Mafumka anasema  wazazi watakapo vuna watapeleka mahindi hayo kwenye uongozi wa sungusungu na wao wataikabidhi shule.

“Mikakati tuliyoiweka nikuhakikisha kila mzazi mwenye mwanafunzi anachangia debe la mahindi  kwa kulileta kwenye uongozi wa sungusungu” anasema  Mafumka.

 Mwenyekiti wa  kitongoji cha Dodoma Maige Robert anasema  wazazi wamekubaliana kuchangia debe moja moja la mahindi shuleni kila mwenye mtoto pindi watakapo vuna.

Maige anasema kitongoji hicho kina wakazi zaidi ya 200 na shughuli zao kuu ni ufugaji na kilimo na suala la elimu kwao sio kipaumbele hawana mwamko.

“Wanafunzi hawapati chakula shuleni  walihamasishwa kwenye mkutano wa hadhara wakadai wataanza kuchangia msimu wa mavuno”anasema  Robert.

Kaimu mtendaji  wa kijiji cha Puni ambaye ni ofisa maendeleo ya jamii wa kata Veronika  George anasema uchangiaji wa chakula shuleni wazazi wanakosa utayari mpaka kupitia jeshi la sungusungu.

“Kijiji cha Puni kina vitongoji 10,kaya 319 na idadi ya watu  kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ni  1595 ambapo  wanaume 638 na wanawake 957”anasema George.

Mtendaji wa kata ya Puni Fumbuka  Mathias anasema kata hiyo ina shule tatu za msingi na zote watoto hawapati chakula shuleni baada ya mkutano  wa hadhara wamekubali kuchangia msimu wa mavuno.

Diwani wa kata ya Puni Heke Salum anasema  alifanya mkutano kwenye kila kijiji nakuahidi kila shule kuchangia gunia moja la mahindi msimu wa mavuno.

Ofisa lishe wa halmashauri ya  wilaya ya Shinyanga   Said Mankilago anasema mwanafunzi akinywa uji wenye sukari inatosha kumpatia nguvu kuliko kukaa bila kula  muda mrefu.

“Kwani tunasisitiza angalau wapate uji shuleni  kwani utatumika unga ambao ni kundi la vyakula vya wanga na sukari itawapa virutubisho  mwilini”anasema  Mankilago.

Mankilago anasema ili chakula   kipatikane  wametumia  jeshi la sungusungu  kuhamaisha  na  kuwekeana  sheria  za uchangiaji  kwani jamii bado haina uelewa juu ya lishe.

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Nice Munisy anasema  kuna shule za msingi 139 na upatikanaji wa chakula shuleni umefikia asilimia 89.

Munisy amewataka madiwani kwenye maeneo yao kuhamaisha wazazi kuchangia chakula shuleni .

Ofisa Elimu mkoa wa Shinyanga Dafroza Ndalichako anasema kuna shule za msingi  za serikali 603 kati ya hizo shule  293 sawa na asilimia  48.5 ndiyo zinatoa chakula shuleni .

“ Jumla  ya wanafunzi   545,339 kwa mkoa mzima wa shule za msingi   na  shule 310 hazitoi chakula shuleni mpaka sasa hivyo jitihada zinafanywa na wazazi kuhakikisha watoto wanapata chakula”anasema  Ndalichako.

Katika program jumuishi ya Taifa ya Malezi ,Makunzi na maendeleo ya Awali ya Mtoto ( PJT-MMMAM) 2021/22 hadi 2025/26 inaeleza afua za lishe hazishughulikii  kwenye elimu ya madarasa ya awali na  kwanza kwa shule za msingi.

Maeneo ambayo yameonekana kuna program  za lishe  shuleni nikutokana  na juhudi  za wadau zinazotokana na ubunifu wao kama sehemu  ya majaribio ya program shuleni.

Aidha lishe hiyo  imeonekana ni uji  ambayo haifikii kiwango cha vyakula bora vyenye mchanganyiko ambapo Taasisi ya chakula na lishe nchini (TFNC)  inaandaa toleo  la kwanza la muongozo wa kitaifa  wa utoaji wa huduma ya chakula na lishe kwa wanafunzi elimu ya msingi.

 

 



 

Post a Comment

0 Comments