Header Ads Widget

MWANAMKE AELEZA JINSI ALIVYOTAKA KUJINYONGA BAADA YA UJAUZITO KUKATALIWA NA MME WAKE



  Suzy Luhende Shinyanga Blog

 

Mwanamke mmoja mkazi wa kijiji cha Mwamakalanga kata ya Iselamagazi wilayani Shinyanga  Rejina Paul ameeleza jinsi alivyobeba ujauzito na  mme wake kuukataa kwamba si wa kwake wa mwanaume mwingine, hali ambayo ilimfanya atake kujinyonga baada ya kukataliwa.

Hayo ameyasema jana Rejina Paul wakati akizungumza na gazeti hili, ambapo alisema kuwa yeye alikuwa mwaminifu kwa mme wake lakini baada ya kubeba ujauzito alishangaa mme wake akikataa  kuwa ujauzito alionao mke wake si wa kwake ni wa mtu mwingine na huku hakusafiri kwenda popote nje ya familia yake.

Amesema aliendelea kuishi na mme wake kwa kuvumilia huku akitukanwa na kupigwa akiambiwa kuwa atoke hapo nyumbani apeleke ujauzito wake kwa mwanaume aliyempa ujauzito, yeye alizidi kukaa hapo hapo lakini alikuwa akiishi kwa kutukanwa kila wakati na wakati mwingine anapigwa kabisa na mme wake.

"Kwa kweli niliteseka sana baada ya kubeba ujauzito wa mtoto wangu kwa jinsi nilivyokuwa nikitukanwa nilitamani nijinyonge kabisa nisionekane tu duniani, lakini baadae nilizungumza na baadhi ya viongozi mbalimbali wa jukwaa la kina mama, wakanitia moyo wakanishauri kuwa nivumilie kweli nilivumilia mpaka nikajifungu mtoto wa kike ambaye alifanana kabisa na baba yake,"amesema Rejina.

"Lakini nilikata tamaa na kusema haya maisha mimi siyataki tena bora nife tu kwa sababu aliyenikataa ndiye aliyenipa ujauzito na ni mme wangu halafu tena ananikana kuwa mimba si yake niliumia sana kwa kweli, lakini namshukuru Mungu baada ya kujifungua mambo yalibadilika mme wangu alimkubali mtoto tukaendelea kuishi kwa amani, hivyo nikajifunza kutochukua maamzi magumu ukiwa na hasira, ameongeza Rejina.

Afisa maendeleo wa kata ya Iselamagazi Joyce Chawala amesema kweli baadhi ya wanawake wamekuwa wakipata changamoto na hii inatokea baada ya mwanaume kupata mwanamke wa nje ndipo husingizia kuwa sio ujauzito wake ili mwanamke huyo aondoke alete mwanamke mwingine.

"Kweli wanawake wanapata wakati mgumu sana wengine wanapigwa hata wakiwa na ujauzito bila kujua kwamba mwanamke anapobeba ujauzito ana kuwa na roho mbili anaweza kufanya maamzi mengine yasiyofaa, kinachotakiwa wanaume acheni kuwafanyia ukatili wanawake wanapokuwa wajawazito nawasipokuwa wajawazito muwe na upendo kwa wenza wenu kwani mliwachagua wenyewe,"amesema Chawala.

Baadhi ya wanaume Charles Jilulu na Majige Salumu walisema hayo wanayafanya baadhi ya wanaume ambao wanakuwa wamewachoka wenza wao na wanakuwa wamesha anzisha mahusiano nje ya ndoa, lakini pia wakati mwingi mwanaume anakuwa amehisi kwamba mke wake alikuwa akitembea na mtu furani ama kambiwa na baadhi ya majirani zake kuwa mke wake ana mahusiano na mwanaume mwingine.

"Naomba kuwashauri tu wanaume wenzangu waache kuwafanyia ukatili wanawake wanapokuwa wajawazito hata kama umehisi kuwa si ujauzito wako tulia mama azae mtaulizana baadae mama akijifungua kuliko kukianzisha wakati akiwa na ujauzito anaweza kuchukua maamzi magumu ambayo yanaweza kusababisha madhara makubwa katika familia,"amesema Juma Mwandu.





Post a Comment

0 Comments