Header Ads Widget

WADAU WAPONGEZA UBORA WA PAMBA MSIMU HUU…BEI IKO POA


Magari yakishusha pamba katika Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU) Mjini Kahama
Pamba ikiwa tayari kwa ajili ya kuipaki


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Wanunuzi wa zao la pamba katika mikoa ya Simiyu na Shinyanga wameeleza kufurahishwa na ubora wa pamba iliyolimwa katika msimu huu hali iliyotokana na usimamizi mzuri wa Serikali kuanzia ngazi ya kijiji kupitia Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS).

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Maafisa Mawasiliano wa Wizara ya Kilimo na Bodi ya Pamba Tanzania, ambao wapo kwenye ziara ya kukutana na wadau wa pamba mikoa inayolima pamba Kanda ya Ziwa, wanunuzi hao wa pamba kutoka Kampuni ya Gaki Investment Ltd , Alliance Ginnery Ltd na Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU) wamesema pamba ya msimu huu wanaikubali sana kwa ubora.

Msimamizi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Manispaa ya Shinyanga, Richard Mugisha amesema Serikali imekuwa macho ‘makini’ sana katika kilimo cha pamba na hivi sasa michezo ya kuchafua pamba kwa kuweka mawe, mchanga, maji, magadi na vitu vingine ili kuongeza uzito havipo hivyo kuifanya pamba kuwa bora.

“Tunaishukuru na kuipongeza sana Serikali kwa usimamizi mzuri wa zao la pamba, imekuwa macho hakuna mchezo wa kuchezea pamba.Na hii ya kutochanganya zao la pamba na mazao mengine imefanya pamba kuwa bora sana. Pamba sasa ni safi sana”,amesema Mugisha.

Ameeleza kuwa ubora huo wa pamba unatokana na usimamizi mzuri katika Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS) na wanunuzi wamekuwa wakinunua pamba kupitia vyama vya Ushirika ili kuwa na uhakika wa ubora wa pamba.

“Licha ya kwamba mwaka jana pamba ilikuwa bora lakini Katika msimu huu pamba ni bora zaidi na kwenye soko la pamba duniani hatujapata malalamiko kuhusu pamba, mambo ni mazuri”,ameongeza.

Naye Mhasibu wa Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd iliyopo katika kijiji cha Kasoli wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, James Mbulu mbali na kuishukuru serikali kwa kuwa na bei elekezi ya pamba ya juu kuliko miaka yote (Sh. 1560 kwa kilo) pia ameipongeza kwa kusimamia zao la pamba vizuri kwa kuhakikisha udanganyifu kwenye mizani unadhibitiwa na pamba inakuwa safi.

“Ubora wa pamba ni mzuri, pamba ikipita kwenye AMCOS inakuwa safi, AMCOS zimeleta nidhamu. Wale mawakala binafsi wa kununua pamba ndiyo wengi wao siyo waaminifu wanachafua pamba na kufanya uchakachuaji wa pamba kwa kuweka mchanga,mawe na maji ili kuongeza uzito wa pamba hali ambayo inachafua pamba”,ameongeza.


“Pamba tunayonunua kwenye AMCOS ni safi, uchafu umepungua sana na hatutumii muda mwingi kutafuta pamba kwa wakulima kama zamani. Wito wetu ni kuhamasisha wananchi kulima kwa tija ili tupate malighafi nyingi kwenye viwanda vyetu na wale wanaoficha pamba majumbani watupe pamba tununue fedha zipo”,amesema Mbulu.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Khamis Majogolo amesema mwaka huu wamepata pamba safi sana kutokana na maandalizi mazuri ya pamba kupitia vyama vya msingi vya ushirika (AMCOS) ambazo zimekuwa zikifuatilia zao pamba kwa umakini mkubwa.

Majogolo ametumia fursa hiyo kuipongeza Serikali kwa kuongeza bajeti katika Sekta ya Kilimo na kuendelea kutoa pembejeo na elimu ya kilimo chenye tija kwa wananchi huku akiwataka vijana kuchangamkia fursa ya ajira katika kilimo kwani Kilimo ni biashara.

“Vijana fumbueni macho, maisha yamehamia kwenye kilimo, njooni huku ili kuondokana na lindi la umaskini, hivi sasa kila zao ni la biashara. Hakuna haja ya kulia lia kuwa hauna ajira kinachotakiwa ni uaminifu, uadilifu na uwajibikaji”,ameongeza Majogolo.

Wanunuzi hao wa pamba wamesema hivi sasa wanaendelea kununua pamba juu ya kiwango cha bei elekezi ya serikali ambayo ni shilingi 1560 kwa kilo moja ya pamba ambapo wao wananunua hadi zaidi ya shilingi 1600 na hivi karibuni bei ya pamba ilipanda hadi kufikia shilingi 2020 kutokana bei kupanda katika soko la dunia.
Mhasibu wa Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd iliyopo katika kijiji cha Kasoli wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, James Mbulu akielezea kuhusu ununuzi wa zao la pamba Julai 13,2022. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Meneja Uzalishaji wa Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd iliyopo katika kijiji cha Kasoli wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, James Muriithi akielezea namna uchambuzi wa pamba unavyofanyika.
Pamba ikiendelea kuchambuliwa katika mitambo
Meneja Uzalishaji wa Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd iliyopo katika kijiji cha Kasoli wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, James Muriithi akielezea namna wanavyopaki pamba baada ya kuichakata.
Pamba iliyozalishwa katika Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd ikiwa tayari kusafirishwa
Muonekano wa sehemu ya mitambo Kampuni ya Alliance Ginnery Ltd
Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Khamis Majogolo akielezea kuhusu zao la pamba na namna wanavyonunua na kuchambua pamba
Magari yakishusha pamba katika Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU) Mjini Kahama
Mhandisi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Himelius Magege akionesha pamba safi wakati akielezea ubora wa pamba waliyonunua katika msimu huu.
Mhandisi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Himelius Magege akionesha pamba ndani ya kiwanda hicho.
Mhandisi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Himelius Magege akionesha pamba iliyochambuliwa katika kiwanda chao.
Kaimu Meneja wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU), Abdul Maiga akionesha pamba iliyochambuliwa katika kiwanda hicho.
Pamba safi iliyopo katika ghala la Kiwanda cha kuchambua pamba cha Chama Kikuu cha Ushirika Kahama (KACU).
Msimamizi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga, Richard Mugisha akionesha pamba safi waliyonunua kupitia Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS).
Uchambuzi wa pamba ukiendelea katika Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga.
Msimamizi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga, Richard Mugisha akionesha pamba safi iliyochambuliwa katika kiwanda chao.
Pamba safi iliyochambuliwa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd ikiondolewa kwenye mitambo tayari kuipaki
Muonekano wa sehemu ya mitambo ya kuchambua pamba katika kiwanda cha Gaki Investment Ltd.
Msimamizi wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga, Richard Mugisha akionesha pamba iliyochambuliwa tayari kwa kuisafirisha.
Meneja wa Kiwanda cha kuchambua pamba cha Gaki Investment Ltd kilichopo Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga, Modest Emmanuel akielezea namna vyama msingi vya ushirika (AMCOS) zilivyosaidia kuwa na ubora wa pamba.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Post a Comment

0 Comments