Header Ads Widget

WANAWAKE WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA ZA KIUCHUMI ILI KUONDOKANA NA UKATILI WA KIJINSIA DHIDI YA WATOTO

 

  Wanawake wa kata ya Masengwa Halmashauri ya wilya ya Shinyanga wakishikiri mafunzo kutoka shirika la WEADO.

 

Afisa maendeleo ya jamii halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Aisha Omary akizungumza na jukwaa la wanawake kata ya Masengwa.


Afisa maendeleo ya jamii  kata ya Masengwa akizungumza na wanafunzi kabla ya uchaguzi wa baraza la watoto.

Afisa miradi wa WEADO Salome Shangari akitoa mafunzo kwa jukwaa la wanawake kata ya Masengwa

 

 Suzy Butondo, Shinyanga

Afisa maendeleo ya jamii wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Aisha Omary amewataka wanawake wa kata ya Masengwa kuchangamkia fursa za kiuchumi zilizopo kijijini hapo,na kuacha kumtegemea mwanaume peke yake hali ambayo itaweza kupunguza matukio ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Pia amewataka kina mama waache kuwaogopa watoto wao katika kuwaonya wakati wanapokosea, badala yake wawafundishe  maadili mema, kuacha kufanya maovu mbalimbali yakiwemo ya kiukatili  wa jinsia, ili kuwa na kizazi chenye amani na utulivu.

Aisha amesema hayo kwenye semina ya kuwajengea uwezo jukwaa la kina mama wa kata ya Masengwa  ili waweze kujishughulisha na kujipatia kipato, na kupunguza matukio mbalimbali ya kikatili yanayofanywa na baadhi ya wanaume, iliyoandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la Women Elderly Advocacy and Development Organization (WEADO),la kutokomeza ukatili wa wanawake dhidi ya watoto.

Amesema matukio ya kupigwa kina mama yamekuwa mengi kutokana na wanawake kuwategemea waume zao kwa kila kitu, ili kuondokana na matukio kama hayo ni vizuri kina mama wakaanza kujishughulisha kwa kulima bustani za mboga mboga na kuzimwagilia kwa sababu wana bwawa ambalo linadumu kwa muda mrefu, kujishughulisha na biashara ndogo ndogo, ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha watoto na kuwafundisha maadili mema.

  " Matukio  matukio ya ukatili wakijinsia yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara kwa sababu mwanamke hana pa kushika lakini kama unajishughulisha utapata chochote na mme wako atapata, hivyo mtachanganya na kuweza kufanya chochote cha kimaendeleo hata mwanaume atakuheshimu hawezi kukupiga tena bila kosa lolote kwa sababu mtakuwa mnaingiza fedha wote,"amesema Omary.

Afisa miradi wa WEADO Salome Shangari , alisema wanawake wakichangamkia fursa ukatili wa kunyanyaswa, kupigwa na kutelekezwa utapungua ama utaisha kabisa kwa sababu kila mmoja atakuwa anaingiza kipato katika majira yote si kusubiri wakati wa kiliomo tu, hivyo ni vizuri mafunzo haya wakayatekeleza wasikae na kusubiri 
matumizi kwa wanaume.

Aidha Afisa tathimini na ufuatiliaji kutoka shirika hilo la WEADO John Eddy alisema licha ya kuchangamkia fursa pia kina mama wanatakiwa kuwakemea watoto ili waache kutenda maovu,kwani mara nyingi wazazi wa kike wanaogopa kuwakemea watoto wanapofanya maovu na kuwaachia wanaume peke yao, hali ambayo imekuwa ikisababisha mtoto kuharibika na kutokuwa na maadili mazuri.

"Pia katika malezi tujitahidi wazazi kuwalea watoto wetu katika maadili mema watoto wetu ni wajanja sana, ukiangalia na huu utandawazi wa tv simu kuna vitu vingine hawatakiwi kuviangalia, tuseme nao tusiwaogope ili wasiige mambo ya wakubwa na kuharibu future yao ya kimaisha"amesema Eddy.

Baadhi ya wanawake waliojiunga kwenye jukwaa la wanawake kata ya masengwa Suzana Dotto amesema wanawake wengi wamekuwa wakiteseka kwa sababu hawana pakushika, wanafanyiwa ukatili wa kupigwa na waume zao wanavumilia tu,lakini kwa sasa kutokana na mafunzo haya kila mmoja ataenda kutoa elimu kwa mwanamke mwenzake ili aweze kujishughulisha kulingana na fursa aliyoko kwenye kijiji chake.

Kwa upande wake mwenyekiti wa jukwaa la akina mama Mwajuma Luchembela mkazi wa kijiji cha Bubale kata ya Masengwa amesema analishukuru sana shirika la WEADO kwa kuwaelimisha jukwaa la wanawake kwani elimu walioipata wanawake itasaidia sana kupunguza ukatili wa kijinsia, wanawake wengi wamekuwa wakiteseka kwa sababu ya kutokuwa na pakushika anategemea apewe matumizi na mwanaume.

"Wengi wetu tunategemea kudaka tu,lakini Mwanamke akiwa na kipato anaweza kumsaidia mme wake amekwama,atamsaidia mtoto kumnunulia madafutari kalamu pamoja na mahitaji mbalimba watasaidizana na wataishi kwa amani na furaha hata chuki hazitakuwepo tena unaamini hilo",amesema Mwajuma.

Leokadia Masegese mkazi wa kata ya Masengwa ambaye ni muhasibu wa jukwaa la wanawake kata hiyo,  amesema wakati mwingine wanaume wanakuwa na hasira kwa sababu hawana hela, hivyo anajua nikifika na furaha nyumbani nitaombwa hela hivyo anakuwa mkali na wakati mwingine kukupiga kwa kisingizio furani ili usimuombe hela hata ya chumvi.

Hata hivyo Shirika la WEADO licha ya kutoa mafunzo kwa jukwaa la wanawake,  pia lilitoa mafunzo kwa baraza la watoto kata ya masengwa na kufanikiwa kuchagua viongozi wa baraza la watoto la kata hiyo,ambapo alichaguliwa mwenyekiti, katibu, mwasibu na wajumbe wa baraza hilo, ambao waliahidi kutoa elimu kwa jamii ili kutokomeza ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.


Mkufunzi akitoa mafunzo kwa wanawake na watoto.

Post a Comment

0 Comments