Header Ads Widget

CHANGAMOTO YA LISHE NI SEHEMU YA UKATILI KWA WATOTO - KATIBU MKUU

 

 



Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mwajuma Magwiza akifungua mafunzo ya Programu Jumuishi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto kwa wataalamu wa Sektetarieri za Mikoa yanayofanyika Jijini Dodoma leo tarehe 11 Desemba, 2021.

 Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya watoto kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Sebastian Kitiku akieleza lengo la mafunzo kuhusu Programu Jumuishi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya mtoto kwa wataalam wa Sektetarieri za mikoa.


 Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya kuhusu programu Jumuishi ya malezi, makuzi na Maendeleo ya awali ya mtoto kwa wataalamu wa Sektetarieri za mikoa yanayofanyika Jijini Dodoma.

Na WAMJW, Dodoma

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Mwajuma Magwiza amesema changamoto ya ukosefu wa lishe bora ni ukatili kwa watoto kwani inawasababishia udumavu wa akili na mwili. 

Magwiza ameyasema hayo tarehe 11,desemba,2021 Jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo kuhusu programu Jumuishi ya malezi, makuzi na Maendeleo ya awali ya mtoto kwa wataalamu wa Sektetarieri za Mikoa nchini yanayofanyika .

Magwiza ameongeza kuwa, jamii haina budi kufahamishwa namna bora ya malezi kwa watoto wao katika kila hatua kitaalam zaidi ili kuwajengea watoto misingi imara ya ukuaji na ujifunzaji.

Amesema pamoja na kuongezeka kwa vitendo vya ukatili kwa watoto vinavyoripotiwa bado ni vichache lakini pia vitendo hivyo vinasababisha ongezeko la udumavu.

"Kuanzisha Kwa programu hii kunawajumuisha wataalamu ikiwemo madaktari ambao wana Sayansi ya malezi makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto hivyo watatusaidia katika kuelimisha Jamii, 
tunajua kila mzazi anaamini anatoa malezi kwa usahihi lakini kuna hatua za malezi za kitaalamu ambazo Jamii zinapaswa kujengewa na washiriki wote humu kutokana na utaalamu wenu. Huduma za malezi zinatakiwa zimjengee mtoto Afya, lishe, ujifunzaji na mwitikio" alisema Magwiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Mtoto Sebastian Kitiku akieleza lengo la programu hiyo alisema washiriki walioalikwa ni muhimu sana katika utekelezaji wake wakiwemo Maafisa lishe, Maafisa elimu, Maafisa Maendeleo na Ustawi wa jamii na Waganga wakuu wa Mikoa. 

"Lengo ni kujenga uelewa wa pamoja kuifahamu programu vizuri ili itapozinduliwa utekelezaji uanze kwa pamoja wote tukiwa na uelewa" alisema Bi Mwajuma

Aidha, vitabu kuhusu programu vimeandaliwa kwa lugha zote mbili lengo pia ni kutekeleza programu hii kwa ujumuishi wake na Uratibu wa pamoja kwa kuingiza kwenye mipango yetu ikiwa ni wakati muafaka wa maandalizi ya bajeti" alisema Kitiku.

Kitiku aliongeza pia programu hiyo inategemea sana ushiriki wa Serikali kwa kuweka utekelezaji katika mipango yake na kushirikiana na Wadau mbalimbali.

Lengo pia ni kukusanya taarifa Kwa kadri inavyowezekana kulingana na viashiria vilivyowekwa kwenye kanzidata na wataalam hao watafundishwa namna ya kukusanya taarifa na kuziingiza kwenye kanzidata hiyo.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo Mwl. Juma Kaponda akizungumza kwa niaba ya washiriki ameishukuru Serikali kwa kuanzisha programu hiyo ambayo itasaidia kutoaelimu kwa jamii ili watekekeleze majukumu ya Malezi kwa watoto.

Kaponda amesema mafunzo hayo yatawajenga na kuwakumbusha umuhimu wa malezi sahihi kwa watoto kwani ni muda mrefu wamekuwa kama wamejisahau. Aidha ameahidi watakwenda kufanya kazi kupitia programu hiyo kwa ufanisi.

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo ya Mtoto imeandaa Programu Jumuishi ya Kitaifa ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto itakayozunduliwa hapo tarehe 13 Desemba, 2021. Programu hii inatekelezwa kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Rais TAMISEMI. 

MWISHO

 

 

Post a Comment

0 Comments