Header Ads Widget

SURUALI YENYE DAMU ILIVYOTENGUA HUKUMU YA ULAWITI SHINYANGA


SURUALI YENYE DAMU ILIVYOTENGUA HUKUMU YA ULAWITI SHINYANGA

Mahakama Kuu ya Masijala Kanda ya Shinyanga, imemuachia huru Daudi Manamba, aliyekuwa anatumikia kifungo cha miaka 30 Jela, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kumuingilia kinyume cha maumbile mwanafunzi wa miaka sita

Mbele ya Jaji Elizabeth Mkwizu, mahakama ilitoa uamuzi huo baada ya kusikiliza rufani iliyokatwa na Manamba akipinga adhabu aliyopewa ya miaka 30 jela na Mahakama ya Wilaya ya Kahama.

Mrufani alipinga adhabu kwa madai kwamba Upande wa Jamhuri hakuthibitisha mashtaka bila kuacha shaka.

Upande wa Jamhuri ukiwakilishwa na Wakili wa Serikali, Enosh Kigoryo, ulidai Jamhuri imethibitisha bila kuacha shaka katika ushahidi wa mashahidi watatu akiwamo baba wa mtoto aliyebakwa.

Ulidai ushahidi unaonyesha tukio lilitokea Januari 21, mwaka 2017, maeneo ya Zongomela wilayani Kahama, baba wa mtoto akidai aliona damu katika suruali ya mtoto na alipomuuliza, alimtaja mrufani kuwa alimbaka.

Inadaiwa mtoto alikuwa akitoka shuleni, akiwa njiani alikutana na mrufani, akampeleka kwenye majani, akamwelekeza ainame, alimvua suruali na kuanza kumwingilia huku akiwa amemziba mdomo na kumtishia kumuua endapo angesema kwa mtu yeyote.

Alidai mtoto alikuwa akilia, lakini mrufani alimziba mdomo na kumtishia, ripoti ya daktari na ushahidi wa uchunguzi ulionyesha alibakwa na sehemu yake ya nyuma ilikuwa wazi kiasi ambacho kitu chochote kinaweza kupita.

Mahakama ya Wilaya iliona mashtaka yamethibitika bila kuacha shaka, hivyo mrufani alitiwa hatiani na kuhukumiwa kwenda jela miaka 30.

Mrufani alipinga adhabu hiyo kwa madai kwamba mashtaka dhidi yake hayakuthibitika.

Mahakama baada ya kusikiliza rufani hiyo, iliikubali hoja za aliyekata rufani kwa kuwa katika ushahidi, ni vigumu kujua tukio lilitokea maeneo gani.

Sababu ya pili, suruali iliyokuwa ikidaiwa kuwa na damu haikutolewa mahakamani kama kielelezo na ushahidi wa upande wa mashtaka haukuwa na nguvu za kuthibitisha mashtaka bila kuacha shaka.

"Kwa kusema hayo, rufani inakubaliwa, adhabu ya miaka 30 jela inafutwa na mahakama inaamuru mrufani aachiwe huru gerezani," alisema Jaji Mkwizu.

Na Kulwa Mzee; Chanzo NIPASHE







Post a Comment

0 Comments