Header Ads Widget

SERIKALI YAIFUNGA SHULE SIKU 14 BAADA YA KUUNGUA MOTO MARA TATU

Baadhi ya majengo ya shule ya sekondari Geita yaliyoungua moto. 

Geita. Serikali imelazimika kuifunga kwa muda wa siku 14 Shule ya Sekondari Geita kutokana na matukio ya kuungua moto mara tatu mfululizo.

Uamuzi huo umetolewa leo Jumatano ya Julai 14,2021 baada ya kuungua moto jana usiku ikiwa ni mara ya tatu ndani ya siku saba. Awali, moto huo ulisababisha uharibifu wa mali, lakini kwenye tukio la jana usiku wanafunzi watatu wamejeruhi.

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Rosemery Senyamule ametangaza uamuzi huo baada ya moto kuteketeza bweni na kujeruhi wanafunzi watatu.

Katika tukio la kwanza lililotokea Julai 5,2021, moto uliteketeza magodoro na masanduku ya wanafunzi, la pili likatokea Julai 6 kwa kuteketeza maabara mbili za sayansi.

Tukio la tatu limetokea usiku wa kuamkia leo na kuunguza vyumba viwili katika bweni la Sokoine na kuunguza magodoro huku mwanafunzi watatu wakijeruhiwa na kulazwa Hospitali ya mkoa wa Geita.

Mkaguzi msaidizi wa zimamoto mkoani hapa Peter Nkwambi, amesema katika tukio hilo mkuu wa shule alipata mshtuko na kukimbizwa katika hospitali ya mkoa.

Geita ni miongoni mwa sekondari kongwe nchini ambayo awali ilikuwa ikimilikiwa na Chama cha Ushirika cha Nyanza kabla ya kuwa chini ya umiliki wa sekondari. Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Godwin Gondwe ni miongoni mwa wanafunzi waliohitimu shuleni hapo.  

 

   Bweni la wanafunzi katika shule ya sekondari Geita ambalo limeteketea kwa moto.

                                                              CHANZO -Mwananchi

Post a Comment

0 Comments