Header Ads Widget

SIMULIZI YA KILIO KWA WATANZANIA 64 WALIOFANYIWA MAJARIBIO YA DAWA YA UKIMWI



Ni nani aliruhusu Watanzania 64 wafanyiwe majaribio ya dawa ya Ukimwi ya Virodene kati ya mwaka 2000 na 2001 licha ya Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) kutotoa kibali?

Je, Watanzania hawa walipewa taarifa sahihi na za kutosha kabla ya kuruhusu miili yao itumike katika majaribio hayo, ambayo matokeo yake hakuna ajuaye hadi leo? Ni nani anastahili kuwajibishwa kwa tukio hilo?

Haya ni baadhi ya maswali yanayodai majibu kuhusu Watanzania hao 64 ambao kati ya mwishoni mwa mwaka 2000 na mwaka 2001 walitafutwa, wakaorodheshwa na kuingizwa katika mpango wa majaribio ya dawa ya Ukimwi iliyoendeshwa nchini na kampuni ya Virodene Pharmaceutical (Pty) Limited ya Afrika Kusini.

Majaribio hayo kama ilivyo kwenye mwenendo wa kesi, yanadaiwa kufanyika katika Hospitali ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) Lugalo na Kituo cha Afya cha Chadibwa, kinachomilikiwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi mstaafu, Omar Mahita, huku yakiacha machungu kwa waliofanyiwa utafiti huo.

Miaka 20 baada ya kufanyiwa majaribio, watu wanaodai kuathirika wameendelea kudai fidia bila mafanikio kutokana na madhara ya kimwili na kijamii waliyoyapata.

Wanadai matumizi ya miili yao kwa majaribio ambayo waligundua hayakuwa na kibali cha Serikali wala viwango vinavyokubalika kisayansi, ulikuwa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na udhalilishaji.

Ingawa Mahakama Kuu imeitupa kesi ya kikatiba waliyofungua mwaka 2014 wakiomba mahakama itamke kuwa majaribio yale yalikuwa kinyume cha ubinadamu, yamewadhalilisha na hayakufuata utaratibu wa kisheria, waathirika hao wameapa kuendelea kupigania haki yao.

Baadhi yao wanadai majaribio yale yaliwasababishia matatizo zaidi ya kiafya, yakiwamo ya ini na tumbo.

“Tunaomba taarifa hizi zimfikie Rais, tunatumai tutapata msaada kutoka kwake, hatua za kiutawala zifanyike, apitie hili jambo kwa undani wake na atusaidie,” anasema mmoja wa waathirika hao, Steven William Kimaro (62).

Licha ya kwamba maombi ya kufanya majaribio ya dawa ya Virodene P058 yalikwishakataliwa katika nchi kadhaa duniani, kampuni hiyo ilifanikiwa kupenya nchini kuendesha majaribio hayo.

Wakati Virodene ikifanyiwa majaribio Tanzania bila kibali cha NIMR, tayari ilikwishakataliwa Uingereza, Ujerumani na Afrika Kusini yenyewe.

SOMA ZAIDI SIMULIZI HII KUPITIA MWANANCHI



Post a Comment

0 Comments