Header Ads Widget

MTENDAJI AGEUKA MBOGO SUNGUSUNGU WALIOTAFUNA FEDHA ZA MADARASA KOLANDOTO...WAZITEMA MMOJA MMOJA


Afisa Mtendaji wa Kata ya Kolandoto Manispaa ya Shinyanga Mwakaluba Wilison, akizungumza kwenye mkutano na wananchi wa kijiji cha Galamba Kata ya Kolandoto kwenye zoezi la kuwabana viongozi wa Sungusungu na kamati nzima juu ya kutafuna fedha za wananchi.

Na Marco Maduhu -Shinyanga. 
Afisa Mtendaji wa Kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga Mwakaluba Wilson, ameendesha msako kwa wajumbe wa Kamati ya Jeshi la Jadi (Sungusungu) katika kijiji cha Galamba kwenye Kata hiyo, ambao wamedaiwa kutafuna fedha za wananchi ambazo walichanga kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya Sekondari ya Kolandoto. 

Msako huo umefanyika leo Jumanne Januari 5,2021 kwenye kijiji hicho, ambapo wajumbe kamati ya Sungusungu walikuwa na fedha za wananchi Shilingi Milioni 5.3, lakini wakazigawana, na walipokuwa wakibanwa kila mmoja alianza kulipa fedha alizokuwa amechukua, na kubaki deni la Shilingi Milioni 3.5 mzigo ambao alibaki nao Katibu wao Mahalu Machimu ambaye amekamatwa na kupelekwa Polisi. 

Akizungumza kwenye zoezi hilo,Wilson amesema hatavumilia viongozi wowote wale ambao wamepanga kukwamisha zoezi la ujenzi wa vyumba vya madarasa, na kutafuna fedha za michango ya wananchi, bali ataendelea kuwachukulia hatua viongozi ambao ni wabadhirifu. 

“Nimesikitishwa sana na uongozi wa Sungusungu kutafuna fedha za wananchi ambazo walichanga kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, na kuanzia sasa ni marufuku Sungusungu kushika fedha mkononi hata iwe ya faini, bali fedha zote zitakuwa zikilipwa kwenye akaunti ambayo nitawafungulieni mimi, ili kuepuka ubadhirifu huu wa fedha,”amesema Wilson. 

“Fedha ambazo zimesalia nataka zilipwe zote, ili tukaezeke majengo yetu ya madarasa katika shule ya Kolandoto, ambapo wanafunzi wamebakiza siku tano tu wafungue shule, na sitakuwa na mchezo kabisa, tutaonana wabaya na hata kama mkinichukia sawa tu, tutakamatana hadi fedha zilipwe,”ameongeza. 

Naye Kamanda mkuu wa Jeshi la Jadi Sungusungu kijijini hapo Paulo Cosmas, ambaye alilipa fedha alizokuwa amezichukua, alisema suala la fedha zilizosalia Shilingi Milioni 3.5 ni mzigo wa Katibu wao, kwa sababu yeye ndiye mwenye nyaraka zote na anafahamu alipozipeleka. 

Kwa upande wake Katibu huyo wa Sungusungu Mahalu Machimu, alikiri ni kweli walikuwa na kiasi cha fedha za wananchi Shilingi Milioni 5.3 lakini fedha hizo zipo kwa wajumbe wengine ambao hawakuonekana kwenye mkutano, pamoja na wengine kukimbia kwenda kujificha, na kuomba muda azifuatilie kwao ili azirejeshe, ombi ambalo liligonga mwamba na kupelekwa Polisi. 

Nao baadhi ya wananchi akiwamo Yohana Kishosha na Kulwa Masanja, wamesema wamesikitishwa sana na kitendo cha uongozi wao wa Sungusungu na kamati nzima kutafuna fedha zao, na kuunga mkono ufunguaji wa akaunti ili fedha ziwe zinawekwa huko, pamoja na kusisitiza viongozi waliosalia kurejesha fedha hizo wabanwe na kuzitoa. 

TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA HAPA CHINI 
Afisa mtendaji wa Kata ya Kolandoto Manispaa ya Shinyanga Mwakaluba Wilison, akizungumza kwenye mkutano na wananchi wa kijiji cha Galamba Kata ya Kolandoto kwenye zoezi la kuwabana viongozi wa Sungusungu na kamati nzima juu ya kutafuna fedha za wananchi. 
Afisa mtendaji wa Kata ya Kolandoto Manispaa ya Shinyanga Mwakaluba Wilison,akisisitiza jambo kwenye mkutano huo. 
Kamanda mkuu wa Jeshi la Jadi Sungusungu kijiji cha Galamba Paulo Cosmas, akitoa majibu kwa wananchi juu ya kugawana fedha za wananchi, ambapo yeye alijinasua kwa kuzilipa fedha ambazo alikuwa amechukua. 
Katibu wa Sungusungu kijiji cha Galamba Mahalu Machimu, akijitetea kwa wananchi kwenye mkutano huo.
Wananachi wakiwa kwenye mkutano.
Mkutano ukiendelea.
Mkutano ukiendelea.
Mkutano ukiendelea.
Mkutano ukiendelea.
Mwananchi Kulwa Masanja akichangia hoja kwenye mkutano huo.
Mwananchi Yohana Kishosha akichangia hoja kwenye mkutano huo.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Sungusungu wakianza kurejesha fedha ambazo walichukua za michango ya wananchi.
Fedha zikiendelea kurejeshwa.

Na Marco Maduhu- Shinyanga.

Post a Comment

0 Comments