Header Ads Widget

WALIOHUSIKA NA MAUAJI YA ALPHONCE MAWAZO WA CHADEMA WAHUKUMIWA KUNYONGWA HADI KUFA

Alphonce Mawazo (aliyeshika kipaza sauti) enzi za uhai wake 

Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita yenye mamlaka ya ziada, imewahukumu watu wanne kunyongwa mpaka kufa baada ya kukutwa na hatia ya mauaji ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Geita na kanda ya Ziwa, Alphonsi Mawazo.

Hukumu hiyo imetolewa leo Desemba 24, 2020 na Hakimu Mkazi Mwandamizi mwenye mamlaka ya ziada na Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Frenk Mahimbari kupitia kifungu namba 197 sura namba 16 marekebisho ya adhabu ya mwaka 2019.

Akisoma hukumu hiyo Hakimu Mahimbari amesema Mahakama imejiridhisha pasi na shaka kuwa washitakiwa wote wanne walikuwepo eneo la tukio kutokana na ushahidi uliyotolewa mahakamani hapo hivyo wamekutwa na hatia ya mauaji ya kukusudia ya kada huyo wa CHADEMA.

Waliohukumiwa katika shauri hilo la mauaji namba 56 la mwaka 2015, ni Alfani Apolinari, Epafura Zakaria, Hashim Sharif na Kalulinde Bwire.

Alphonsi Mawazo ambae alikuwa pia mgombea wa jimbo la Busanda mkoani Geita aliuawa siku chache baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 katika mji wa Katoro.

Post a Comment

0 Comments