Header Ads Widget

KITILA MKUMBO, WASSIRA, MAKONDA, MSANDO, KANGI LUGORA NAO WAJITOSA VITA YA UBUNGE



Mwanasiasa mkongwe na Waziri wa zamani katika serikali za awamu zilizopita, Stephen Wassira amechukua fomu ya kuomba kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea ubunge Jimbo la Bunda Mjini mkoani Mara.

Na Shinyanga Press Club Blog
Orodha ya wanasiasa, viongozi wa Serikali na watu mashuhuri wanaojitokeza kuchukua fomu za kugomba ridhaa ya kuteuliwa kuwa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika majimbo mbalimbali nchini inazidi kuongezeka.

Baada ya zoezi la uchukuaji fomu kufunguliwa rasmi jana Julai 14, 2020 ndani ya chama hicho na kushuhudiwa majina mbalimbali mashuhuri na yasiyodhahaniwa, orodha imeendelea kuwa ndefu leo Julai 15, 2020 ambapo pia yameshuhudiwa majina mengine makubwa ya wanasiasa na viongozi wa serikali wakijitokeza kuchukua fomu hizo.

Miongoni mwa waliojitokeza leo ni Steven Wassira, Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Prof. Kitila Mkumbo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugora, aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Benjamin Sitta, Muandaaji maarufu wa Muziki wa Bongofleva, 'Master Jay' pamoja na Wakili Albert Msando.

TAZAMA PICHA ZAIDI

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amechukua fomu ya kugombea ubunge Jimbo La Kigamboni, Dar es Salaam.

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola leo amechukua fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea ubunge katika Jimbo la Mwibara mkoani Mara.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Prof Kitila Mkumbo leo amechukua fomu ya kuomba uteuzi wa CCM kugombea ubunge Jimbo la Ubungo.

Aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Uwekezaji Nchini (TIC), Geofrey  Mwambe amechukua fomu kugombea kiti cha ubunge jimbo la Masasi mkoani Mtwara kwa tiketi ya CCM.

Mtayarishaji maarufu wa muziki wa Bongofleva na mmiliki wa studio za M Jay, Joachim Marunda Kimaryo maarufu kama ‘Master Jay’ naye amechukua fomu kugombea Ubunge katika Jimbo la Rombo mkoani Kilimanjaro.

 Wakili Maarufu nchini, Albert Msando naye amejitokeza leo kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya CCM kumteua kuwa mgombea wa ubunge Jimbo la Arusha Mjini.