.jpg)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewaapisha rasmi majaji tisa wa Mahakama Kuu waliopandishwa cheo kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.
Akizungumza mara baada ya uapisho huo, Rais Samia amewataka majaji hao kutekeleza majukumu yao mapya kwa kuzingatia uzalendo wa hali ya juu na kuweka mbele maslahi ya Taifa.
Amewakumbusha kuwa uhuru wa mahakama una thamani kubwa pale tu unapoenda sambamba na uadilifu, ufanisi, na maamuzi yanayotanguliza nchi kwanza kabla ya mambo mengine yote.
Katika hotuba yake kwa viongozi hao wapya wa ngazi ya juu ya utoaji haki, Mkuu wa Nchi amewahimiza kwenda kuitumikia nchi kwa weledi na uadilifu kama walivyoapa, akisisitiza umuhimu wa kutoa maamuzi bila upendeleo, huba, wala chuki.
Amewataka majaji hao kujitathmini kwa kina katika kutoa hukumu zao na kutambua kuwa dhamana waliyopewa si ya cheo tu, bali ni wajibu mkubwa wa kulinda na kusimamia haki za Watanzania.
Rais amesisitiza kuwa uamuzi wanaoutoa una uzito mkubwa unaoathiri taasisi, mwenendo wa jamii, na tafsiri pana ya sheria nchini, akiongeza kuwa wanapohudumia wananchi kwa haki wanakuwa wanatumikia kazi ya Mungu pia.
Rais Samia amebainisha kuwa uteuzi wao umetokana na uzoefu, weledi, na utumishi mzuri waliouonesha katika nafasi zilizopita, jambo lililofanya Tume ya Utumishi wa Mahakama kutambua mchango wao na kuwapendekeza kupandishwa cheo.

Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za makusudi za kufanya maboresho na kuimarisha uwezo wa mhimili wa mahakama nchini ili kukabiliana na ongezeko la mashauri na kukidhi mahitaji ya wananchi kwa wakati.
Baada ya maboresho hayo ya miundombinu na mifumo, Rais ameeleza kuwa kazi iliyopo sasa ni kuongeza nguvu kazi ya watu wenye dhamira, uwezo, na msimamo thabiti wa kusimama kwenye mstari sahihi wa haki ili kulinda heshima, nidhamu, na maadili ya mhimili huo muhimu.
Majaji walioapishwa kuingia rasmi kwenye majukumu hayo mazito ya Mahakama ya Rufani ni Mhe. Imani Daud Aboud, Mhe. Rabia Hussein Mohamed, Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Mhe. Immaculata Kajetan Banzi, Mhe. Cyprian Phocas Mkeha, Mhe. Yohane Bokobora Masara, Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo, Mhe. Abdi Shaaban Kagomba, na Mhe. Mzee Ibrahim Ibrahim.