Baada ya mazungumzo ya muda mrefu, mradi wa kielelezo na kimkakati wa Liganga na Mchuchuma sasa upo tayari kwa utekelezaji.
Kwa mujibu wa Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani Njombe majadiliano sasa yamefikia asilimia 90 huku Serikali ikiwa imeshalipa shilingi bilioni 15 kama fidia kwa wananchi kupisha mradi huo.
Mradi huu unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi kwa kutoa ajira za moja kwa moja zipatazo 6,500 na ajira zisizo za moja kwa moja takriban 26,000.
Aidha uwekezaji wake unakadiriwa kuwa kati ya dola bilioni 2 hadi 3.
Katika mradio huo mgodi wa chuma wa Liganga utakuwa na uwezo wa kuzalisha malighafi ya tani milioni 2.9 kwa mwaka, wakati mgodi wa makaa ya mawe wa Mchuchuma utazalisha tani milioni 3 kwa mwaka na kuendesha kituo cha kufua umeme cha megawati 600, hatua itakayozalisha mapato ya jumla ya zaidi ya Shilingi trilioni 5.175 kwa Serikali katika kipindi cha miaka 25 ya kwanza.







