Header Ads Widget

TIMU YA RIADHA YA BARRICK NORTH MARA YAITANGAZA TANZANIA MASHINDANO YA CAPE TOWN MARATHON


Kapteni ya timu ya Barrick North Mara Runners Club, Sarah Cyprian, akifurahi baada ya kumaliza mbio za kilometa 42.2 za CapeTown Marathon zilizomalizika nchini Afrika ya Kusini Karibuni.

 

Kapteni ya timu ya Barrick North Mara Runners Club, Sarah Cyprian, akifurahi baada ya kumaliza mbio za kilometa 42.2 za CapeTown Marathon zilizomalizika nchini Afrika ya Kusini Karibuni.
Kapteni ya timu ya Barrick North Mara Runners Club, Sarah Cyprian, akifurahi baada ya kumaliza mbio za kilometa 42.2 za CapeTown Marathon zilizomalizika nchini Afrika ya Kusini Karibuni.
Timu ya riadha ya Barrick North Mara Runners Club, inayoundwa na wafanyakazi wa mgodi wa Barrick North Mara, baada ya kushiriki mashindano mbalimbali ya ndani sasa imezidi kuchanja mbuga na kushiriki mashindano ya Kilometa 42.2 ya Sunlam Cape Town Marathon yaliyomalizika nchini Afrika ya kusini karibuni ambapo pia imepata fursa ya kuitangaza Tanzania katika mashindano hayo.

Kapteni ya timu hiyo, Sarah Cyprian,ameeleza kuwa wachezaji wote wa timu hiyo wako vizuri na wameweza kushiriki mbio hizo za umbali mrefu na kumaliza,na kudai kuwa wamefurahi kushiriki katika mashindano hayo makubwa ya riadha ya kimataifa na kuitangaza Tanzania.

Alisema katika mashindano hayo ambayo yamewakutanisha wakimbiaji kutoka nchi mbalimbali wamejifunza mambo mengi na anaamini wameanza kupata uzoefu utakaowawezesha kufanya vizuri zaidi katika mashindano ya kimataifa watakayoshiriki siku za mbele.

Sarah alieleza kuwa timu ya riadha ya Barrick North Mara Runners Club, ilianzishwa mwaka 2016 na inajumuisha wakimbiaji 66,miongoni mwao Wanaume wapo 53 na Wanawake 13.

Alisema baadhi ya mashindano ambayo klabu hiyo imeshiriki ameyataja kuwa ni Kilimanjaro International Marathon -Moshi, Capital City Marathon -Dodoma(ilitoa mshindi wa tisa wa umbali wa kilometa 21 ) , Serengeti Migration marathon 21km-Mugumu, Serengeti Safari Marathon 21km-Lamadi na Lake Victoria Marathon -Mwanza (ilitoa mshindi wa 4 kwa wanawake umbali wa kilometa 21).

Mashindano makubwa ambayo timu hiyo imeshiriki na kung’ara ameyataja kuwa ni Kilimanjaro International Marathon ambapo ilishiriki mbio za kilometa 21 na kilometa 42.Kwa mbio hizo za masafa marefu ya kilometa 42 klabu iliwakilishwa na yeye mwenyewe. (Sarah Cyprian).


Akielezea siri ya mafanikio ya klabu Sarah alisema “Kampuni ya Barrick inayo sera mathubuti katika kusaidia wafanyakazi kwenye upande wa michezo. Kwanza kwa kuwa na miundo mbinu ya mazoezi kama gym, swimming pool, uwanja wa mpira wa miguu , uwanja wa mpira wa kikapu pamoja na uwanja wa mpira wa pete. Pia inatoa vifaa na nyenzo mbalimbali za kufanyia mazoezi, vilevile kugharamia huduma zote tunapoenda kwenye mashindano nje”.


Aliongeza kusema kuwa Kampuni pia kupitia kitengo cha Afya na Usalama huwa inaandaa mashindano ya ndani kwa kushindanisha idara mbali mbali hii ni kama njia moja wapo yakuweza kuweka vizuri afya za mwili na akili za wafanyakazi wawapo kazini.


Kuhusu ni jinsi gani wanaweza kutenga muda wa kazi na muda wa kufanya mazoezi Sarah alisema “ Kila mtu ana masaaa 24 katika siku.Klabu ya North Mara Runners huwa tunatenga muda wa saa moja katika siku kufanya mazoezi.Mazoezi hayo huwa tunafanya jioni mara baada ya kutoka kazini,na mara chache ratiba zinapokuwa zinabana jioni huwa tunafanya mazoezi saa kumi alfajiri kabla ya kwenda kazini”.


Kuhusiana na changamoto wanazokutana nazo katika mazoezi na kushiriki mashindano alisema kulingana na majukumu ya kazi huwa kuna wakati ni vigumu wote kwenda kushiriki mashindano, lakini huwa wanajitahidi kutoa wawakilishi kwa ajili ya kushiriki mashindano, na kampuni huwa inawaunga mkono wakati wote.


Akitoa maoni kuhusu maendeleo ya tasnia ya mchezo wa mbio za marathon nchini alisema katika miaka ya hivi karibuni kumekuwa na mwitiko mkubwa katika mchezo wa mbio na kushauri kuwa ni vizuri kuanza maandalizi mapema kwa vijana wadogo ili kuweza kuwa na washiriki wengi katika mbio za kimataifa.Aliongeza kusema kuwa kuna wakimbiaji wengi wenye vipaji nchini kwa sasa ambao wanashiriki mashindano ya marathon mbalimbali yanayoandaliwa nchini.


Sarah, alitoa wito kwa jamii kujitahidi kutenga muda hata nusu saa kwa siku kufanya mazoezi. “Mazoezi yanasaidia kuimarisha afya ya akili na mwili. Pia mazoezi yanasaidia kuweza kujikinga na magonjwa yasioambukiza kama kisukari, shinikizo la damu na unene wa kupindukia”alisema.


Kuhusu malengo ya baadaye ya klabu hiyo alisema “Kauli mbiu ya club yetu ni ‘We run for fun and healthy’ hivyo basi bado tunajukumu la kuhimiza wafanyakazi wengi zaidi kufanya mazoezi kwa ajili ya afya zetu, kwani mazoezi pia yamekuwa yakituweka vizuri kiakili hata kuweza kutimiza majukumu yetu kazini kwa ufanisi zaidi.Lakini pia kuweza kushiriki zaidi katika marathoni za kimataifa.”

Wachezaji wa timu ya Barrick North Mara Runners Club, wakifurahia baada ya kumaliza mbio ndefu za kilometa 42.2 katika mashindano ya Cape Town Marathon yaliyomalizika hivi karibuni nchini Afrika ya Kusini
Wachezaji wa timu ya Barrick North Mara Runners Club, wakifurahia baada ya kumaliza mbio ndefu za kilometa 42.2 katika mashindano ya Cape Town Marathon yaliyomalizika hivi karibuni nchini Afrika ya Kusini

Post a Comment

0 Comments