Header Ads Widget

MWANAFUNZI DARASA LA TANO SHINYANGA AJINYONGA BAADA YA KUMALIZA KUNYWA CHAI


Picha siyo ya tukio halisi

Na Halima Khoya, SHINYANGA 
 
MWAFUNZI wa darasa la tano shule ya msingi Ndala ‘A’ Manispaa ya Shinyanga Brayton Daniel (11) amekutwa amejinyonga kwa kamba nyuma ya mlango nyumbani kwao.

Tukio hilo limetokea Oktoba 26 mwaka huu majira ya saa 4 asubuhi, nyumbani kwao Mtaa wa Mwabundu Kata ya Ndala Manispaa ya Shinyanga.

Akisimulia tukio hilo jana mama mkubwa wa marehemu Joyce Kalulu, amesema mtoto huyo hakuwa hana tatizo lolote, lakini siku hiyo walipomaliza kunywa chai, yeye aliondoka kwenye mihangaiko yake ya maisha na aliporudi nyumbani majira ya saa 8 mchana akakuta mlango umefungwa kwa ndani, walipovunja wakamkuta kijana amefariki kwa kujinyonga.

“Asubuhi nimeamka na kufanya kazi zote nikawa nimewaacha kijana wangu na bibi yake, nimerudi saa 8 kutoka kazini nikamkuta mama anahangaika kumuita Brayton afungue mlango, ndipo tulipoamua kwenda kumuita Mwenyekiti ambaye alifanikiwa kutoboa nyavu za dirisha na kumuona Brayton akiwa amening’inia mlangoni,”amesema Kalulu.
 
Naye Mwenyekiti wa Mtaa wa Mwabundu Pili Masanja amesema taarifa za tukio hilo alizipata majira ya saa 9 mchana, na alipofika kwenye familia hiyo ikabidi watoboe nyavu ya dirisha alipochungulia akamuona mtoto huyo akiwa amening'inia nyuma ya mlango.

“Majira ya saa 9 alikuwa mama mkubwa mtoto huyu kuniita nikawasaidie kufungua mlango nilipofika ambapo nilizunguka nyuma yumba ili kutoboa dirisha lakini nilichokiona baada ya kutoboa dirisha ni Brayton akiwa amejinyonga na kamba  kwenye mlango, ndipo nikapiga simu Polisi,”amesema Masanja.

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la polisi Mkoa Shinyanga Janeth Magomi, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo huku akibainisha kuwa Jeshi hilo bado linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo cha tukio hilo.

Post a Comment

0 Comments