Header Ads Widget

WAKUU WA WILAYA WAKARIBISHWA RASMI SHINYANGA...RC SENGATI ATAKA WASIMAMIE MAENDELEO

 

Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa kuwakaribisha Mkoani Shinyanga Wakuu wa Wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko) na Kahama (Festo Kiswaga) ambao wameteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati amewakaribisha na kuwatambulisha mkoani Shinyanga Wakuu wa Wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko) na Kahama (Festo Kiswaga) ambao wameteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Dkt. Sengati amewakaribisha Wakuu hao wa wilaya leo Jumatatu Juni 21,2021 katika hafla fupi ya kutambulisha viongozi hao iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ikihudhuriwa na viongozi wa serikali na wadau mbalimbali wa serikali.

“Tumekutana hapa kwa ajili ya kuwakaribisha Wakuu wa wilaya walioteuliwa na Mhe. Rais. Hatutafanya zoezi la kuwaapisha kwa sababu hawa wamehamishwa tu maeneo ya kazi na mkuu wa wilaya ya Shinyanga anaendelea kutumikia nafasi hiyo katika wilaya hiyo hiyo. Karibuni sana Ma DC wapya tufanye kazi katika mkoa huu wa kimkakati”,amesema Dkt. Sengati.

Mkuu huyo wa mkoa pia ametumia fursa hiyo kuwashukuru waliokuwa Wakuu wa wilaya ya Kishapu (Nyabaganga Talaba) na Kahama (Anamringi Macha) kwa kazi nzuri za kizalendo walizozifanya katika kuwaletea maendeleo wananchi.

“Wakuu wa wilaya nyinyi ndiyo wasimamizi wakuu wa shughuli zote za maendeleo.Mkuu wa wilaya ni kiongozi mkuu wa serikali katika wilaya na ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama. Mna wajibu wa kwenda popote , naomba mzingatie sheria kanuni na taratibu”,amesema Dkt. Sengati.

“Mkatatue changamoto za wananchi bila kuchoka, nawajua nyinyi ni wachapakazi, naomba muendeleze mazuri ya mkoa wa shinyanga.Mkasimamie halmashauri katika kusimamia mipango mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kusimamia utu, uwajibikaji na utawala bora. Naomba tuache alama nzuri ya kukumbukwa na wananchi kwa kuzingatia utumishi mzuri”,ameongeza.

Dkt. Sengati pia amewataka Wakuu wa wilaya hao kuepuka kubeza kazi za watangulizi wao huku akiwasisitiza kuwa wabunifu.

“Wapo baadhi ya watu wao kazi yao ni kubeza kazi za waliowatangulia, Msiende kubeza kazi zilizofanywa na watangulizi wenu. Mkatambue kazi zilizofanywa na watangulizi wenu, mje na ubunifu katika kuwaletea maendeleo wananchi ,kwani Shinyanga tumepiga hatua kimaendeleo”,amesema Dkt. Sengati.

“Matarajio yetu ni makubwa sana kwenu , naamini mtasimamia biashara na uwekezaji ikiwemo kulinda wawekezaji wadogo, tunataka kuona wilaya zenu zinapaa kiuchumi.Tubuni pia vyanzo vipya vya mapato huku tukiendelea kuimarisha umoja na mshikamano katika kada mbalimbali ili tufanye kazi kama timu, tuweke pembeni masuala ya fitina na majungu”,ameongeza Dkt. Sengati.

Katika hatua nyingine amewataka kwenda kudhibiti upigaji katika miradi ya maendeleo akisema hataki kuona ubadhirifu kwenye miradi ya maendeleo na fedha za umma.

“Mimi sitakuwa kikwazo kwa maendeleo ya mkoa wa Shinyanga lakini pia Ma DC pia msiwe vikwazo. Sitavumilia watumishi na viongozi ambao kwa maksudi au hulka zao wanazorotesha maendeleo. tutawashughulikia wanaokwamisha maendeleo ya mkoa wa Shinyanga”,amesisitiza Mkuu huyo wa Mkoa.

“Pelekeni huduma stahiki kwa wananchi, tatueni kero za wananchi, tokeni ofisini, msikae kwenye viyoyozi, kasikilizeni na kutatua kero za wananchi,ongeeni na makundi mbalimbali ya wananchi. Hatutamani mkoa huu uwe mkoa wa matukio mabaya, bali tunataka mkoa wenye matukio mazuri”,amesema.

Aidha amewasihi kuendelea kuimarisha zaidi mahusiano mazuri ya Chama Cha Mapinduzi na serikali akibainisha kuwa ni lazima viongozi wa chama waheshimike na wapewe ushirikiano na viongozi wa serikali.

Kwa upande wao waliokuwa Wakuu wa wilaya za Kishapu (Nyabaganga Talaba) na Anamringi Macha (Kahama) wamesema wataendelea kuwa wananchi wema na kuzingatia mamlaka, sheria, taratibu na kanuni zote katika kulijenga taifa

“Tunaahidi utiifu kwa Rais Samia, tutatambua mamlaka zilizopo wakati wote na tupo tayari kutoa ushirikiano kwa viongozi walioteuliwa na Mhe. Rais. Tunawapongeza sana mlioteuliwa na Mhe. Rais, tunatambua uchapakazi wetu hivyo tunawatakieni majukumu mema”, amesema Anamringi Macha.

“Sisi tuliongoza na kuna mahali tulifikia na nyinyi mtaanzia hapo tulipoishia. Naamini na nyinyi mtaenda kutuongoza kulingana na mazingira yaliyopo nasi tunaahidi kuwa tutaendelea kushirikiana na viongozi wote wakiongozwa na Rais wetu Mpendwa Mhe. Samia Suluhu Hassan.

“Najua sasa kazi kubwa iliyopo mbele yenu ni Mbio za Mwenge wa Uhuru, tunaomba tuwakabidhi jezi za kupokelea Mwenge wa Uhuru mkoani Shinyanga ili kazi iendelee”,ameongeza Macha.

Naye aliyekuwa Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Talaba amewaomba Wakuu wa wilaya walioteuliwa kusimama imara katika kutekeleza majukumu yao akieleza kuwa wataendeleza pale walipoishia.

“Tumeacha mauaji ya vikongwe yameisha, mimba za watoto zimepungua, tumepunguza changamoto ya upungufu wa madarasa, tumeacha watu wanafanya kazi na mambo mengine kadha wa kadha, nendeni mkaendeleze pale tulipoishia katika kuwatumikia wananchi wa Shinyanga. Mkoa upo vizuri, msiache maombi, msiache kuiombea serikali yetu na Rais wetu Mhe. Samia Suluhu” ,amesema Talaba.

Kwa upande wao, Wakuu wa wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko ) na Kahama (Festo Kiswaga) wamemshukuru Mhe. Rais Samia kwa kuendelea kuwaamini kutumikia nafasi hizo huku wakiahidi kwenda kuwatetea watu maskini kwa nguvu zangu zote ili kujenga uchumi.

“Wananchi wa Shinyanga wanataka kuona maendeleo, tutahakikisha tunabadilisha mkoa. Tunaamini kabisa kuwa kazi zitaendelea katika mkoa wa Shinyanga, tunaomba kupatia ushirikiano tu katika kufanikisha mambo yote mazuri tunayotaka mkoani Shinyanga”,wamesema.

Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa kuwakaribisha Mkoani Shinyanga Wakuu wa Wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko) na Kahama (Festo Kiswaga).
Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa kuwakaribisha Mkoani Shinyanga Wakuu wa Wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko) na Kahama (Festo Kiswaga) ambao wameteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa kuwakaribisha Mkoani Shinyanga Wakuu wa Wilaya za Kishapu (Joseph Modest Mkude), Shinyanga (Jasinta Mboneko) na Kahama (Festo Kiswaga) ambao wameteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Joseph Modest Mkude (kushoto), Shinyanga Jasinta Mboneko (kulia) na Kahama Festo Kiswaga wakiandika dondoo muhimu wakati Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu Mhe. Joseph Modest Mkude akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa hafla fupi kukaribishwa Mkoani Shinyanga 
Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga  akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa hafla fupi kukaribishwa Mkoani Shinyanga 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza leo Jumatatu Juni 21,2021 wakati wa hafla fupi kukaribishwa Mkoani Shinyanga 
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Joseph Modest Mkude (kushoto), Shinyanga Jasinta Mboneko (kulia) na Kahama Festo Kiswaga wakifurahia jambo ukumbini.

Post a Comment

0 Comments