Header Ads Widget

RAIS SAMIA SULUHU APIGILIA MSUMARI KWA WENYE MASHAKA NAYE

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akilihutubia Taifa katika Viwanja vya Jamhuri Mjini Dodoma ambako kumefanyika ibada ya kutoa heshima na kuaga mwili wa mpendwa wetu Hayati Dk.John Pombe Magufuli aliyefariki Dunia Machi 17 mwaka huu katika Hospitali ya Mzena ,Dar es Salaam.

Na Kadama Malunde
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu amewahakikishia Watanzania kuwa hakuna jambo litakaloharibika kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwatoa hofu baadhi ya watu wanaosema kuwa mwanamke anaweza kweli kuongoza nchi au la.

Mhe. Samia Suluhu Hassan ameyasema hayo leo Jumatatu Machi 22,2021 wakati akiongoza viongozi mbalimbali na wananchi kuaga mwili wa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli katika uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Amesema mtangulizi wake huyo amemuachia mema yatakayokumbukwa wakati huu na vizazi vijavyo ikiwemo utendaji kazi wake ambao aliona muda wa saa 24 kwake haukuwa ukimtosha.

Kiongozi mkuu huyo wa nchi amewataka Watanzania wenye mashaka watambue aliyesimama uwanjani hapo ni rais licha ya kuwa yeye ni mwanamke.

Amesema yuko imara kutokana na namna alivyolelewa na mtangulizi wake huyo kwa hiyo haoni kama kuna mahali watu wanaweza kuwa na hofu naye.

"Na hapa nataka niseme kidogo kwa wale ambao wanamashaka kuwa Mwanamke huyu ataweza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nataka niwaambie kuwa aliyesimama hapa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye maumbile yake ni mwanamke",amesema Rais Samia.

"Daima Nitamshukuru Rais Magufuli kwa imani yake kubwa kwangu na kwa wanawake wa Tanzania, Tukiandika historia ya usawa au uwiano wa kijinsia kwenye nyanja za siasa nchini lazima Magufuli jina lake litakuwemo .Na kupitia yeye Tanzania ilipata Mwanamke wa kwanza Makamu wa Rais na sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

"Nafarijika alinipa fursa ya kuonesha uwezo wangu na kuwa wanawake tunaweza tukijengewa mazingira ya kufanya kazi kisawa sawa. Inanipa faraja kuwa kwa takribani miaka sita nilihudumu kama msaidizi wake wa kwanza na wa karibu"

"Hakuna jambo litakaloharibika nchi yetu ipo salama, tutaendeleza alipoishia na tutafika alipopatamani tufike",ameongeza.

Post a Comment

0 Comments