Header Ads Widget

MTOTO AFARIKI NA WENGINE WAWILI WAZIRAI BAADA YA KUNYWA DAWA YA KIENYEJI KUSAFISHA NYOTA


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba akizungumza leo na waandishi wa habari mjini Shinyanga (hawapo pichani)

Na Damian Masyenene
Mtoto mmoja aliyejulikana kwa jina la Juma Dela Megejua (12) Mkazi wa Mwaningi Kata ya Bulige Tarafa ya Busangi Halmashauri ya Msalala mkoani Shinyanga amefariki baada ya kunywa dawa ya mitishamba idhaniwayo kuwa na sumu ili asafishwe nyota yake.

Marehemu pamoja na wenzake wawili waliotambulika kwa majina ya Loya Nsalala Ngusa (66) ambaye ni jirani wa mtuhumiwa na Bahati Ludahila Ngusa (25) mkazi wa Shilima Kwimba mkoani Mwanza ambaye ni mgeni aliyefikia nyumbani kwa mtuhumiwa, walipewa dawa hiyo na Mganga wa jadi aitwaye Juma Dela Megejua (44) ambaye ni baba wa mtoto aliyefariki.

Akisimulia tukio hilo wakati akitoa taarifa kwa Waandishi wa habari Ofisini kwake leo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba amesema tukio hilo lilitokea Januari 16, mwaka huu saa 9:30 Alasiri kijijini hapo, ambapo Marehemu (Juma) ambaye ni mtoto wa mtuhumiwa alifariki dunia baada ya kunywa dawa hiyo ya kienyeji inayodhaniwa kuwa sumu akiwa na watu wawili nyumbani kwa mtuhumiwa ambao walikunywa dawa hiyo na kuzirai papo hapo na kukimbizwa kituo cha afya Chela kwa matibabu na hali zao zinaendelea vizuri.

RPC Magilimba ameeleza kuwa mtuhumiwa alikimbia mara baada ya tukio hilo na kwamba jeshi hilo linamtafuta kufuatia kusababisha kifo cha mwanae na kujeruhi (kusababisha maumivu) kwa watu wengine wawili.

Kamanda huyo amesema kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya halmashauri ya Mji wa Kahama kwa uchunguzi zaidi.

"Natoa Wito wa waganga wa jadi mkoa wa Shinyanga kuwa na uhakika na matumizi ya dawa zao pamoja na matumizi mazuri ya vibali/leseni zao ili kuepuka kusababisha vifo na madhara kwa wateja wao. Na jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga halitamuonea muhari mganga yeyote anayekwenda kinyume na maelekezo ya vibali/leseni zao," amesisitiza.

Mkoa wa Shinyanga unatajwa kuwa na utamaduni wa wanajamii kuwasafisha nyota watoto hususan wa kike ili kuwaondolea mikosi na kufanya wapendwe na wanaume na kuolewa mapema. Utamaduni ambao unapingwa vikali na wanaharakati wa masuala ya ukatili wa wanawake na watoto.

Ambapo, tukio hilo linatokea ikiwa ni miezi michache tu baada ya Mkoa wa Shinyanga kuzindua mpango mkakati wa miaka mitano (2020-2025) wa kutokomeza ukatili wa kijinsia, ambapo zoezi hilo lilifanyika katika halmashauri ya Msalala ambako tukio hilo limetokea, huku wilaya ya Kishapu nayo ikitajwa kuendekeza utamaduni huo wa kusafisha nyota watoto.

Post a Comment

0 Comments