Header Ads Widget

TCRS YAWAWEZESHA AJIRA VIJANA ZAIDI YA 200 KIJIJI CHA MIPA KISHAPU KUPITIA MRADI WA KILIMO RAFIKI

Vijana waliokuwa wakiishi katika maeneo yenye ukame Kijiji cha Mipa wilayani Kishapu ambao wamenufaika na mradi wa kilimo rafiki wa mazingira na ukuzaji uchumi kwa kutumia teknolojia rahisi ya umwagiliaji kwa njia ya matone, wakiendelea na shughuli za umwagiliaji shambani.

Na Mwandishi wetu, Kishapu
Vijana zaid ya 200 wasiokuwa na ajira na wanaoishi katika maeneo yenye ukame wilaya ya kishapu mkoani shinyanga wameondokana na changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa ajira baada ya wadau wa maendeleo mkoani humo kuanza kutekeleza mradi wa kilimo rafiki wa mazingira na ukuzaji uchumi kwa kutumia teknolojia rahisi ya umwagiliaji kwa njia ya matone hali ambayo imetajwa kuwa imeanza kubadilisha staili ya maisha ya vijana hao waliokuwa na hali ngumu ya maisha. 

Vijana hao kutoka katika Kijiji cha Mipa Kata ya Sekebugolo Wilayani kishapu, vijana hawa waliokuwa hawana ajira kwa muda mrefu wanaeleza hali ilivyokuwa ngumu awali na sasa baada ya mradi huo unaotekelezwa na Shirika linalojihusisha na Utunzaji wa Mazingira na Upatikanaki wa Maji Safi na Salama (TCRS) kwa ufadhili wa Shirika la Norwegian Church Aid (NCA) la nchini Norway. 

Fortina Boniface ni kijana mmojawapo ambaye amenufaika na mradi huo amesema awali maisha yalikuwa ni magumu lakini baada ya shirika la tcrs kuanza kutekeleza mradi huo na kuwapa nyenzo mbalimbali kama bitendeakazi maisha yao yameanza kubadilika na uchumi wa mtu mmoja mmojaffamilia na vikundi nao umepata sura mpya ya matumaini. 

Mwanamina Jumanne ni Afisa Mradi kutoka Shirika la Kimataifa la Tanganyika Christian Refugee Service (TCRS) linalojihusisha na utunzani wa mazingira na upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo yenye ukame ikiwemo wilaya ya kishapu amesema lengo la kupeleka mradi huo wa kilimo rafiki wa mazingira na ukuzaji wa uchumi ni kuwakwamua vijana na wanawake ambao walikuwa hawana ajira na mradi unatekelezwa katika kata mbili wilayani kishapu mojawapo ikiwa mi sekebugolo.

Ameeleza kuwa pamoja na mradi huo miradi mingine inayotekelezwa kwa ajili ya ukuzaji wa uchumi wa wakazi wa maeneo hayo ni ufugaji wa kuku na ufugaji bora wa nyuki pamoja na kazi mbalimbali za mikono kama kutengeneza batiki na kushona vikapu vunavyotumika badala ya mifuko ya plastiki iliyokuwa imepigwa marufuku kwa sababu ya uharibifu wa mazingira. 

Nao wadau wengine kutoka makao makuu ya TCRS Dar-Es-Salaam, Lukundo Zawadi ambaye ni Afisa Mhamasishaji wa vijana na Kellen Mmachibya wamesema malengo ya shirika la TCRS kuleta miradi ya umwagiaji kwa njia rahisi na yakisasa, ufugaji wa kuku na nyuki pamoja na utengenezaji wa batiki, sabuni na vikapu ni kuwasaidia wananchi zaidi sana vijana kujikwamua na umasikini na kutoka katika maisha tegemezi kwa wazazi na ndugu zao. 

Naye Afisa Miradi wa Shirika la TCRS Kata ya Sekebugolo, Frank George Nyumbeleka amesema mradi huo wa kilimo rafiki wa mazingira na ukuzaji wa uchumi katika kata hiyo ulianza mwezi wa nane mwaka huu katika vijiji vitatu ambavyo ni mipa,mwamasololo na durisi kwa kuwapa vijana waliojiunga katika vikundi vitendeakazi pamoja na mbegu na mbolea vikiwemo vifaa vya umwagiliaji kwa njia ya matone na mwitikio wa vijana umekuwa mkubwa kuliko matarajio yalivyokuwa. 

Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa Wilaya ya Kishapu, Diwani Kata ya Sekebugolo, Fredinand Mpogomi amelishukuru shirika la TCRS kusaidia vijana na jamii ya watu wa kishapu akidai kuwa ukame na uhaba wa maji ni changamoto kubwa inayowakabili wananchi huku akiwataka vijana kuacha tabia ya kukimbilia mijini badala yake wakungane na vijana wenzao katika miradi rafiki ambayo imeanzisha na shirika hilo. 
Afisa Mitaji TCRS Makao Makuu Dar es Salaam, Kellen Mmachibya 
Afisa Mhamasishaji wa vijana kutoka TCRS, Lukundo Zawadi 
Afisa Mradi kutoka Shirika la Kimataifa la Tanganyika Christian Refugee Service (TCRS), Mwanamina Jumanne 
Afisa Miradi wa Shirika la TCRS Kata ya Sekebugolo, Frank George Nyumbeleka akizungumzia namna vijana wa kijiji cha Mipa walivyonufaika na mradi wa kilimo unaotekelezwa na Shirika hilo
Wanakijiji walionufaika na ajira katika mradi huo wa kilimo wakionyesha mashamba yao
ukaguzi wa miundombinu inayotumia teknolojia rahisi ya umwagiliaji kwa kutumia matone, ikikaguliwa na maofisa kutoka TCRS
Mashamba yanayotekeleza mradi huo yakikaguliwa
Baadhi ya mazao yanayolimwa katika mradi huo


Vijana hao wakiendelea na shughuli za shambani katika mradi wa kilimo unaotekelezwa na shirika la TCRS

Post a Comment

0 Comments