Header Ads Widget

MTANDA AFUNGWA MIAKA 30 KWA KUMBAKA BINTIYE WA MIAKA 11



CHANZO: Nipashe
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Singida, imemhukumu kifungo cha miaka 30 jela mkazi wa Mtaa wa Kimpungua, Manispaa ya Singida, Hamisi Mtanda (37) kwa kosa la ubakaji.

Mtanda amehukumiwa kifungo hicho baada ya mahakama kumtia hatiani kwa kosa la kufanya mapenzi na mtoto wake wa kike, mwenye umri wa miaka 11.
 
Ilidaiwa na Mwanasheria wa Serikali, Elizabeth Barabara, kwamba mshtakiwa alianza kufanya mapenzi na mtoto wake huyo (jina linahifadhiwa) kuanzia Julai, mwaka jana, kwa kumchokonoa kwa vidole baada ya kutengana na mama wa mtoto huyo.
 
Mwanasheria huyo alidai kuwa mshtakiwa alitengana na mke wake, ambaye ni mama mzazi wa mtoto, Modesta Mshana na hivi sasa anaishi mkoani Dar-es-Salaam na alikwenda kumchukua mtoto huyo akiwa na umri wa miaka sita na kuanza kuishi naye.
 
Barabara alidai kuwa katika kipindi chote hicho, mshtakiwa huyo kabla ya kuanza kumwingilia kimwili mtoto ambaye ni mwanafunzi (jina la shule linahifadhiwa), alikuwa akimnyemelea usiku akiwa amelala.
 
Alidai kuwa mshtakiwa baada ya kuona sehemu za siri za mtoto zimetanuka, ndipo alipoanza kumwingilia kimwili na wakati akifanya unyama huo, mtoto alikuwa akipiga kelele za kuomba msaada bila mafanikio kutokana na maumivu aliyokuwa akiyapata.
 
Mwanasheria huyo alidai kuwa, kutokana na mshtakiwa kukana shtaka la kutenda kosa hilo, upande wa Jamuhuri ulipeleka mashahidi sita, akiwamo daktari ambaye alithibitisha bila kuacha shaka yoyote kwamba mshtakiwa ndiye aliyemwingilia mtoto huyo.
 
Kutokana na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka, mahakama ilijiridhisha bila kuacha shaka yoyote kuwa mshtakiwa huyo ndiye aliyemfanyia unyama huo mtoto wa kumzaa mwenyewe.
 
Kabla ya kutolewa adhabu, mshtakiwa alipewa nafasi ya kujitetea kwa kudai kuwa hakufanya unyama huo bali mtoto huyo alikuwa amefanya vitendo vya ngono na mwalimu, bila kumtaja ni mwalimu yupi.
 
Akitoa hukumu, Hakimu Mkazi Mwandamizi Robert Oguda, alisema anamhukumu mshtakiwa kifungo cha miaka 30 jela, ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama za mshtakiwa huyo.

Post a Comment

0 Comments