Header Ads Widget

TAMWA ZANZIBAR YATOA MAFUNZO YA UFUGAJI WA KUKU KWA WAHANGA WA VITENDO VYA UDHALILISHAJI





Na Gaspary Charles - Zanzibar
CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) - Zanzibar kimewapatia mafunzo ya ufugaji wa Kuku Wanawake 10 walioathirika na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia ikiwemo utelekezaji kisiwani Pemba.

Mafunzo hayo ya siku moja  yaliyojumuisha waathirika wa vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia kutoka Wilaya ya Wete na Mkoani yamelenga kuwawezesha wanawake kujuendeleza kiuchumi baada ya kukumbana na udhalilishaji huo.

Mratibu wa Chama hicho Ofisi ya Pemba, Fat-hiya Mussa Said amesema lengo la kutolewa kwa mafunzo hayo ni kuwawezesha Wanawake kujisimamia kiuchumi baada ya kukumbwa na udhailishaji ikiwemo utelekezaji.

“Tumebaini kwamba sababu kubwa ya kuwepo kwa wimbi la ubakaji na udhalilishaji katika jamii chanzo chake ni mifarakano ya kifamilia na utelekezaji, hivyo TAMWA Zanzibar imeamua kuandaa mafunzo haya ili yawasaidie wahanga wa vitendo hivyo kujishughulisha katika shughuli mbalimbali za kiuchumi,” Alisema.

Naye mwezeshaji wa mafunzo hayo, Omar Hamad Mjaka amesema mafunzo hayo yamekikita kuwapatia mbinu mpya za ufugaji wa kisasa ili uweze kuwasaidia kuimaisha vipato vyao na kujikimu kiuchumi.

“Mafunzo haya yanalenga kuwapatia elimu na mbinu mpya za ufugaji wa Kuku kwa kutumia njia bora za kisasa na kuondokana na ufugaji wa mazoea kwa lengo la kukuza uchumi wa familia.” alisema.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Riziki Said Khatib ameishukuru TAMWA Zanzibar kwa kuwezesha mafunzo hayo na kwamba yatawasaidia kujikwamua kiuchumi kutokana na hali ngumu ya maisha wanayokabiliana nayo.

 “Tunashukuru sana kwa mafunzo haya, tunaamini kupitia ufugaji itatuwezesha kujisimamia wenyewe na kuendesha familia zetu ikiwa ni pamoja na kuwasomesha watoto wetu.” alisema.

Utoaji wa mafunzo hayo kwa Wanawake ni utekelezaji wa mradi wa Jukwaa la wanahabari la kumaliza vitendo vya udhalilishaji Zanzibar unaotekelezwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake TAMWA, Zanzibar kwa ufadhili wa Danish International Development Agency (DANIDA).